🚨Ni katika kuendeleza Sekta za Mafuta na Gesi.
🚨Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi wafikia asilimia 47.
Na Lubango Mleka, Dar es Salaam.
NCHI za Tanzania na Uganda zitaendelea kushirikiana katika uendelezaji wa miradi mbalimbali ya Nishati ikiwemo Sekta ya Mafuta na Gesi ambapo Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi umefikia asilima 47.
Hayo yamesemwa leo Novemba 22, 2024 jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio wakati akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya kushiriki Jukwaa la Kibiashara kati ya Tanzania na Uganda.
"Tunaangalia ni kwa jinsi gani Sekta hii ya Mafuta na Gesi inaweza ikachangia katika maendeleo ya Nchi hizi mbili, tumekuwa na mijadala mbalimbali inayolenga kuiendeleza sekta hii ya mafuta na gesi." Amesema Dkt. Mataragio.
Ameongeza kuwa, mjadala mkubwa katika jukwaa hilo ni kuangalia namna gani nchi za Tanzania na Uganda zinaweza kushirikiana katika sekta za mafuta na gesi.
Mataragio amesema kuwa, Tanzania na Uganda zinahistoria ndefu za mashirikiano akitolea mfano mradi wa kimkakati wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi wa EACOP.
Akiuelezea mradi huo wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi (EACOP), Dkt. Mataragio amesema umefikia asilimia 47.
Amesisitiza kuwa, mradi huo kwa sasa upo katika hatua ya kutandaza mabomba ambapo takribani kilomita 52 za mabomba zimesha chomelewa ambazo zitaanza kufukiwa ardhini.
Akizungumzia faida ya mradi kwa wananchi amesema watanzania wameweza kujengewa uwezo (Capacity building) katika maeneo mbalimbali na hivi sasa wanafanya kazi kwenye mradi huo.
Kwa upande wa ajira mradi huo umeweza kutoa zaidi ya ajira 8000 huku lengo likiwa ni kutoa ajira 10,000.








Comments
Post a Comment