Fresha Kinasa-Mara.
WAZAZI na walezi wametakiwa kuendelea kuweka misingi bora ya elimu kwa Watoto na kuwalinda dhidi ya vitendo vya Ukatili wa Kijinsia ili wasome na kufikia ndoto zao.
Hayo yamesemwa Novemba 22, 2024 na Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Hope for Girls and Women in Tanzania (HGWT) linalojishughulisha na kutetea haki za Wanawake na Watoto Mkoa wa Mara Rhobi Samwelly wakati akizungumza katika mahafali ya sita kwa wahitimu wa Elimu ya Awali ya pili katika Shule ya Msingi St. John Bosco iliyopo Mjini Musoma Mkoa wa Mara.
Akisoma hotuba yake Rhobi amesema, ili Watoto wafike mbali kielimu Wazazi na walezi wanalojukumu la kuhakikisha wanaimarisha misingi bora kwa watoto wao kuanzia nyumbani ikiwemo kuhakikisha wanakuwa na nidhamu ya kupenda kusoma, kufuatilia maendeleo yao kitaaluma, na kushirikiana na Walimu wao kwa ukaribu.
Aidha, mewahimiza Wazazi na Walezi kusimamia malezi na makuzi bora ya watoto na kuwajenga katika mafundisho ya kiroho na kuwaombea kwa Mungu ili wafanikiwe kwa uwezo mkubwa kwa manufaa ya Jamii na Taifa pia.
"Tukemee pia vitendo vya ukatili wa Kijinsia kwa Watoto wetu, na pia tuwalinde, tuweni makini na waangalizi wa Watoto wetu pamoja na kuachana na mila na desturi mbaya dhidi ya watoto ukiwemo ukeketaji, ulawiti, vipigo visivyo na utaratibu. Lengo ni kuona Watoto wanasoma vyema na kufika mbali zaidi kwa manufaa yetu na Jamii pia."amesema Rhobi.
Akisoma risala ya shule hiyo Mwalimu Mkuu Msaidizi Simon Machango amesema, shule hiyo ilianzishwa rasmi na Shirika la Liones Club mwaka 1985, kama shule ya awali na mwaka 1993, shule hiyo ilikabidhiwa rasmi kwa Jimbo la Musoma chini ya usimamizi wa Masista wa Moyo Safi wa Maria Africa.
Ameongeza kuwa, Uongozi wa Masista uliifanya shule hiyo iwe ya kwanza kujulikana kama shule binafsi inayotoa huduma stahiki. Huku pia wakiiendeleza shule hiyo ya awali kuwa Msingi.
Amesema, jumla ya Wahitimu wa elimu hiyo ni 34, ambapo wavulana ni 17, na Wasichana wakiwa ni 17. Huku pia akitaja mafanikio kuwa ni pamoja na watoto kuwa na uwezo wa kusoma na kuandika kabla ya kuingia darasa la kwanza, madarasa yenye mazingira sanifu ya kujifunzia, vitabu vya kutosha vya kiada, kompyuta kwa ajili ya wanafunzi kujifunzia, Walimu mahiri na wenye weledi.
Rhobi amekabidhi msaada wa vifaa vya michezo ukiwemo mpira, na akabasi 30 kwa ajili ya wanafunzi kujifunzia shuleni hapo.








Comments
Post a Comment