SHULE ya Sekondari Mwembeni mkoani Mara imepata msukumo mpya wa kuinua kiwango cha taaluma baada ya Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mara, Mhe. Agnes Marwa, kukabidhi projector ya kufundishia pamoja na taulo za kike kwa wanafunzi wa shule hiyo, huku akiwataka wanafunzi kujituma katika masomo na kuwa walinzi wa amani ya Taifa.
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi Projector ya kufundishia pamoja na Taulo za Kike katika shule ya sekondari Mwembeni, Mhe. Agnes Marwa Mbunge viti Maalumu Mkoa wa Mara, amesema ndoto yake ni kuona Shule ya Sekondari Mwembeni ikitajwa miongoni mwa shule zinazofanya vizuri kitaifa, akisisitiza kuwa mafanikio hayo yatapatikana kupitia nidhamu, juhudi na kujituma kwa wanafunzi.
"Natamani sana kuisikia Mwembeni iking'ara kitaifa. Ninyi ndiyo mtakaolibeba na kulipandisha jina la shule yenu. Kumbukeni kuwa elimu mnayoipata ni uwekezaji wa maisha yenu wenyewe, hivyo jitumeni kwa bidii ili kutimiza ndoto zenu," amesema Mhe. Agnes.
Mhe. Agnes amesema msaada alioutoa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za walimu na wanafunzi katika kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji, huku akiahidi kuendelea kushirikiana na shule hiyo kila pale atakapopata uwezo.
Aidha, amewahimiza wanafunzi kuendelea kuenzi na kuilinda amani ya Tanzania, akisema maendeleo ya elimu, uchumi na ustawi wa jamii hayawezi kupatikana bila utulivu.
"Tuwafundishe watoto wetu uzalendo na kuipenda nchi yao. Mambo ya kisiasa yabaki kwenye siasa, lakini suala la kuilinda Tanzania ni jukumu la kila mmoja. Huwezi kuiharibu nchi yako kwa mikono yako mwenyewe halafu utegemee maendeleo," amesisitiza.
Nao baadhi ya walimu katika shule hiyo wamempongeza Mhe. Agnes Marwa kwa moyo wake wa kujitoa kusaidia sekta ya elimu, akisema amekuwa mfano wa viongozi wanaoweka mbele maslahi ya wanafunzi na walimu huku wakisema kuwa projector waliyopewa itarahisisha ufundishaji kwa kutumia teknolojia ya kisasa, hatua itakayoongeza ufanisi wa walimu na kuwasaidia wanafunzi kuelewa masomo kwa urahisi zaidi.
"Tunakushukuru kwa kutusogezea teknolojia hii muhimu. Pia tunakupongeza kwa kuendelea kutetea maslahi ya walimu bungeni, hususan wakati wa mjadala wa bajeti ya Wizara ya Elimu. Tunakuona ukiwa sauti ya walimu na mdau mkubwa wa maendeleo ya elimu," wamesema walimu
Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mwembeni walieleza furaha yao kwa msaada huo, wakisema projector hiyo itaboresha mazingira ya kujifunzia huku taulo za kike zikiwasaidia wanafunzi wa kike kuhudhuria masomo kwa utulivu na kujiamini zaidi.
Mwanafunzi Christina James amempongeza Agnes Marwa kwa kuwajali wanafunzi na kutambua mahitaji yao muhimu, huku Lucas Tumaini akiahidi kuwa wanafunzi wa Mwembeni wataongeza bidii katika masomo ili shule hiyo izalishe wanafunzi wengi watakaofaulu kwa kiwango cha juu na kuendelea kuitangaza Mwembeni kitaifa.





Comments
Post a Comment