WIZARA ya Maji imewasilisha vipaumbele na mwelekeo wa sekta ya maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni mkakati wa Serikali kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na salama unaongezeka nchini kote, hususan vijijini na mijini.
Akizungumza leo Mei 5,2026 Bungeni Jijini Dodoma wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Maji Kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 Waziri wa Maji, Mhe. Juma Aweso amesema Wizara itaendelea kuimarisha usimamizi wa rasilimali za maji ili kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi wote na kuendana na mahitaji ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
“Wizara itaendelea kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa rasilimali za maji ili kuhakikisha upatikanaji wa maji kwa wananchi na shughuli za maendeleo,” amesema Mhe. Aweso.
Wizara imesema itaendelea na utekelezaji wa Mpango Kabambe wa Taifa wa Maji pamoja na Gridi ya Taifa ya Maji ambayo inalenga kusafirisha maji kutoka vyanzo vikuu kama maziwa na mito kwenda maeneo yenye uhaba mkubwa wa maji nchini.
Katika kuongeza uhakika wa maji, Wizara itaimarisha uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa kuendeleza ujenzi na ukarabati wa mabwawa 33, kufanya usanifu wa mabwawa mapya 34, pamoja na kufanya tathmini ya mazingira kwa mabwawa mawili, huku pia ikihamasisha wananchi kutumia mifumo ya kuvuna maji ya mvua majumbani.
Wizara pia imeeleza kuwa itaweka msukumo katika kukamilisha miradi ya maji inayoendelea ili wananchi waanze kunufaika kwa wakati, ambapo miradi ya maji vijijini 992, mijini 196 pamoja na miradi ya usafi wa mazingira 26 inatarajiwa kukamilishwa.
Aidha, Serikali imepanga kupeleka huduma ya maji katika vijiji 314 kati ya vijiji 1,575 ambavyo bado havijafikiwa na huduma hiyo, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kuhakikisha kila Mtanzania anapata maji safi na salama.
Amesem Wizara pia itaendelea kudhibiti upotevu wa maji kwa kutumia teknolojia za kisasa kama mita za kielektroniki, mifumo ya kidijitali ya usimamizi wa maji, dira za malipo kabla na ukarabati wa miundombinu ya maji, huku hatua kali za kisheria zikichukuliwa dhidi ya uharibifu na wizi wa miundombinu.
Katika kuimarisha huduma kwa wananchi, Serikali imesema itaendelea kuhakikisha maji yanapatikana katika shule na vituo vya afya ili kuboresha mazingira ya afya, usafi na huduma kwa wananchi, huku pia ikishirikiana na wadau mbalimbali katika utekelezaji wa miradi hiyo.
Kwa upande wa uendeshaji wa sekta, Wizara imesema itatumia vyanzo mbalimbali vya fedha ikiwemo Hati Fungani (Bonds), ushirikiano na sekta binafsi, pamoja na fedha za mabadiliko ya tabianchi na Mfuko wa Taifa wa Maji ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maji nchini.
“Lengo letu ni kuhakikisha uwekezaji katika sekta ya maji unaleta tija na unawanufaisha wananchi wote,” amesema Mhe. Aweso.
Wizara ya Maji imesisitiza kuwa vipaumbele hivyo vinalenga kuhakikisha maji yanakuwa ya uhakika, endelevu na yanawafikia Watanzania wote bila ubaguzi.




Comments
Post a Comment