WAZIRI wa Kilimo, Daniel Chongolo, anatarajiwa kutangaza bei elekezi ya Serikali kwa zao la pamba kesho Mei 10, 2026, katika uzinduzi rasmi wa msimu wa ununuzi wa pamba wa mwaka 2026/2027 utakaofanyika Kijiji cha Mwamashimba, Wilaya ya Igunga mkoani Tabora.
Uzinduzi huo wa Kitaifa unaosimamiwa na Bodi ya Pamba Tanzania (TCB), umeamsha matarajio makubwa kwa maelfu ya wakulima wa zao hilo la kimkakati, huku wengi wakisubiri kwa hamu kusikia bei mpya itakayotoa mwelekeo wa msimu mpya wa kilimo na biashara ya pamba nchini.
“Bei ya pamba ndiyo moyo wa mkulima, ikipewa thamani nzuri inaongeza nguvu ya uzalishaji na kuleta matumaini mapya ya maendeleo kwa familia nyingi,” amesema mmoja wa wakulima waliozungumza na waandishi wa habari za pamba na mazingira waliowasili wilayani Igunga.
Wakulima hao wameeleza kuwa zao la pamba limeendelea kuwa uti wa mgongo wa uchumi katika maeneo mengi ya uzalishaji, wakiamini kuwa tangazo la Serikali litakuwa chachu ya kuongeza ari ya kilimo, tija na kipato kwa wananchi wanaotegemea zao hilo.


