SERIKALI imeendelea kufungua ukurasa mpya wa maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini baada ya kuanzisha miradi mbalimbali ya matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kilimo, afya na ufugaji, huku Tanzania ikiendelea kupata heshima kubwa katika majukwaa ya kimataifa kupitia UNESCO.
Akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma leo Mei 7, 2026, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema Serikali imeanzisha miradi ya kisasa ya nyuklia inayolenga kuongeza uzalishaji wa mazao, kuboresha tiba ya saratani na kuinua sekta ya mifugo.
Prof. Mkenda amesema kupitia Tume ya Nguvu ya Atomu Dar es Salaam, Serikali imeanza mradi wa utunzaji wa mazao kwa njia ya mionzi, huku Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Zanzibar (ZARI) ikiendesha mradi wa kuboresha mbegu ya mpunga kwa teknolojia ya nyuklia ili kukabiliana na ugonjwa wa mabaka ya mpunga na kuongeza uwezo wa mbegu kuvumilia chumvi.
Katika sekta ya afya, alisema Serikali imepanua huduma za tiba ya saratani kwa kutumia mionzi katika Taasisi ya Saratani Ocean Road, Hospitali ya Bugando, KCMC, Benjamin Mkapa pamoja na Hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar.
“Serikali imeendelea kutumia sayansi na teknolojia ya nyuklia kuongeza tija katika sekta za kilimo, afya na ufugaji kupitia utekelezaji wa miradi ya kimkakati,” amesema Prof. Mkenda.
Amesema Serikali pia imeanzisha mradi wa kuimarisha huduma za uhimilishaji kwa njia ya bandia na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kuongeza uzalishaji wa ng’ombe wa maziwa kupitia Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo.
Katika hatua nyingine, Serikali imeanza kutumia mbinu ya kuachilia wadudu dume tasa kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao ikiwemo inzi wa matunda, hatua inayotajwa kuongeza usalama wa chakula na tija kwa wakulima.
Prof. Mkenda amesema kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO, Serikali imeanza utekelezaji wa Programu ya BRIDGE Tanzania 2025–2029 inayowapa vijana waliokosa elimu rasmi nafasi ya kupata ujuzi na stadi za maisha katika wilaya za Masasi, Geita na Kaskazini “A” Unguja, ambapo vijana 200 tayari wamenufaika.
Aidha, amesema Tanzania imeendelea kung’ara kimataifa baada ya kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Kimataifa la Uratibu la Programu ya Mtu na Mazingira ya UNESCO pamoja na Kamati ya Urithi wa Dunia kwa kipindi cha 2025–2029.
“Uteuzi huo umeongeza hadhi ya Tanzania duniani na kufungua zaidi fursa za uhifadhi wa mazingira, urithi wa dunia na maendeleo endelevu,” amesema.
Prof. Mkenda amesema Serikali imewasilisha UNESCO maombi ya kuanzisha hifadhi mbili za miamba duniani katika maeneo ya Arusha na Kilimanjaro kutokana na urithi wake mkubwa wa kijiolojia wenye thamani ya kimataifa.
Pamoja na hayo, Serikali imeendelea kutoa elimu dhidi ya ukatili wa kijinsia mtandaoni katika vyuo mbalimbali mkoani Morogoro, ambapo zaidi ya wanafunzi 1,200 wamefikiwa kupitia semina na kampeni za uhamasishaji kuhusu matumizi salama ya majukwaa ya kidijitali.

Comments
Post a Comment