Akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma leo Mei 25, 2026, Katambi amesema kasi ya usajili imeongezeka ambapo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026 pekee, NIDA ilisajili watu 1,145,334 wenye umri wa miaka 18 na kuendelea, ikilinganishwa na 844,994 katika kipindi kama hicho mwaka uliopita.
Amesema mafanikio hayo yamechochewa na maboresho ya huduma pamoja na upanuzi wa wigo wa usajili, ikiwa ni sehemu ya kufikia lengo la sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022.
Katika huduma kwa Watanzania waishio nje ya nchi, amesema jumla ya wananchi 156 wamesajiliwa kupitia balozi za Tanzania nchini Canada, Marekani, Uingereza na Umoja wa Falme za Kiarabu, na kufanya jumla ya Watanzania 1,465 walioko nje ya nchi kunufaika na huduma hiyo tangu mwaka 2023.
Kwa upande wa Namba za Utambulisho wa Taifa (NIN), Katambi amesema watu 857,244 walipewa namba hizo katika kipindi hicho, na kufanya jumla ya waliopata NIN kufikia 22,654,206, hatua inayowezesha upatikanaji wa huduma za kijamii na kiuchumi kwa urahisi zaidi.
Aidha, amesisitiza waajiri wote nchini kuhakikisha wanatumia mfumo wa NIDA kuthibitisha taarifa za waajiriwa wao ili kuongeza uaminifu na kuimarisha usalama wa taifa.
Kuhusu vitambulisho vya taifa, amesema jumla ya vitambulisho 232,535 vimechapishwa na kusambazwa katika ofisi za wilaya za NIDA, huku 275,682 vikiwa vimekabidhiwa kwa wananchi. Hadi sasa, vitambulisho vilivyokwisha gawiwa ni 20,894,235 kati ya 21,563,057 vilivyochapishwa.
Hata hivyo, amesema bado kuna vitambulisho 668,822 ambavyo havijachukuliwa na wananchi katika ofisi za NIDA wilayani, licha ya jitihada za Serikali kusogeza huduma karibu na wananchi na kuanzisha mfumo wa SMS kuwataarifu wahusika.
Amesema vitambulisho hivyo ni muhimu kwa kupata huduma mbalimbali ikiwemo bima ya afya, ruzuku za kilimo, mikopo ya TASAF na taasisi nyingine za kifedha, pamoja na kutumika kama nyaraka rasmi za utambulisho.
Katika kuboresha huduma, Katambi amesema NIDA imeanzisha namba ya bure ya SMS 15274 itakayowawezesha wananchi kufuatilia hatua za maombi yao ya vitambulisho na kupata taarifa za NIN bila kufika ofisini.
Aidha, Serikali imetoa fursa maalum ya mwaka mmoja kuanzia Oktoba 2025 hadi Septemba 2026 kwa wananchi kurekebisha taarifa zisizo sahihi zilizopo kwenye mfumo wa NIDA. Hadi Aprili 2026, maombi 873 ya marekebisho yameshughulikiwa.
Katambi amewahimiza wananchi kutumia fursa hiyo muhimu ili kuhakikisha taarifa zao ni sahihi na zinakidhi matumizi ya huduma mbalimbali za kitaifa.

Comments
Post a Comment