Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, akiwasilisha Bungeni jijini Dodoma Mei 22, 2026, amesema Serikali imeendelea kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia nchini kupitia Mamlaka ya Ushindani (FCC) pamoja na taasisi nyingine husika.
Amesema hadi Aprili 2026, FCC ilitekeleza operesheni maalum katika maeneo mbalimbali, hususan mkoa wa Dar es Salaam, ambapo jumla ya chupa 4,251 za vinywaji bandia zilikamatwa, pamoja na chupa tupu 286 na katoni tupu 250.
Katika operesheni hiyo, pia vifaa vya uzalishaji na ufungashaji wa bidhaa hizo vilikamatwa, vikiwemo mashine za kuchapisha maelezo ya bidhaa, kipima kilevi, mashine za kufunga vifuniko, mizani, ethanoli pamoja na vifaa vya kuchanganyia na kuchujia pombe.
Aidha, FCC imebaini uwepo wa bidhaa nyingine bandia za vipuri na vilainishi, ambazo pia zilikamatwa, huku wahusika wakichukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa sheria.
Waziri Kapinga amesema Serikali imeweka mkakati madhubuti unaolenga kuimarisha uchunguzi wa kiintelijensia, kuongeza operesheni za ukaguzi na ukamataji, pamoja na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wahusika wa biashara haramu ya bidhaa bandia.
Kwa upande mwingine, kupitia Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Serikali imebaini ongezeko la unywaji holela wa pombe unaoweza kusababisha athari za kiafya, kiuchumi na kijamii.
Katika mwaka wa fedha 2025/2026, TBS imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya pombe zilizo bora na salama, ikishirikiana na sekta za Afya na Maendeleo ya Jamii katika mikoa ya Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Dodoma na Mwanza.
Serikali imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha bidhaa zote zinazotumika nchini zinakidhi viwango vya ubora na usalama kwa afya na ustawi wa wananchi.

Comments
Post a Comment