NA: MWANDISHI WETU, PANGANI
Timu zote 16 zilizoshiriki mashindano ya mpira wa miguu ya Aweso Vijana Cup 2026, zimeneemeka kushiriki mashindano hayo. Hii inatokana na uamuzi mfadhili wa mashindano hayo ambaye ni Mbunge wa Pangani na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, kuamua kupeleka tabasamu kwa timu zote.
Katika hotuba yake aliyoitoa Mei 16, 2026, katika uwanja wa Kumba wilayani Pangani, siku ya fainali iliyozikutanisha timu za Kata za Bweni na Kimang'a, Aweso ameahidi kuzipa zawadi timu zote zilizoshiriki mashindano hayo.
"Ndugu zangu, nazipongeza timu za Bweni na Kimang'a kwa mechi nzuri iliyokuwa na ushindani mkubwa katika fainali hii. Pamoja na hayo, naahidi kuzipa timu zote zilizoshiriki mashindano haya shilingi 500,000, jezi seti moja na mpira ili kuendeleza kukuza michezo wilayani kwetu," amesema Aweso.
Maamuzi haya ni motisha kwa wachezaji wa timu zilizoshiriki mashindano hayo kuendelea kucheza kwa bidii ili kukuza vipaji vyao.
Katika mashindano hayo, timu 16 zilizoshiriki ni pamoja na timu kutoka Kata za Bweni, Ubangaa, Mwera, Kimang'a, Mkaramo, Masaika na Mikinguni
Timu nyingine ni Madanga, Mkwaja, Bushiri, Kipumbwi, Tungamaa, Pangani Mashariki na Magharibi, VETA na Watumishi.
AWESO VIJANA CUP IJAYO USIPIME
Katika kuchagiza maendeleo ya michezo wilayani humo, Aweso ametangaza donge nono katika mashindano yajayo.
"Aweso Vijana Cup hii ilikuwa ni ya maandalizi tu, mashindano yajayo mshindi wa kwanza atapata milioni kumi na mshindi wa pili milioni tano, siitaki zawadi za mbuzi," amesema Aweso
WANAWAKE WAKUMBUKWA KATIKA MICHEZO
Aweso ameahidi kufadhili mashindano ya wanawake katika mchezo watakaochagua wenyewe, na mshindi wa mashindano hayo atapata milioni kumi na mshindi wa pili milioni tano.
Katika pambano la fainali ya Aweso Vijana Cup 2026, timu kutoka Kata ya Bweni iliibuka mshindi kwa kuifunga Kimang'a kwa mikwaju ya penati (5-4).





Comments
Post a Comment