MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Mara, Mhe. Ghati Zephania Chomete, ameibana Serikali kuhakikisha fedha zilizoombwa na Wizara ya Kilimo zinatolewa kwa wakati ili kutekeleza miradi ya kilimo kwa ufanisi.
Akichangia Bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Aprili 28, 2026, katika Bunge la 13 jijini Dodoma, Mhe. Chomete alisisitiza kuwa bila uwekezaji wa kutosha, sekta ya kilimo haiwezi kuleta mageuzi yanayotarajiwa kwa wakulima.
“Kilimo ni zaidi ya chakula; ni biashara na ajira. Tukikifadhili ipasavyo, tutainua maisha ya wananchi wetu.”
Katika hoja yake, alielekeza pia umuhimu wa kufufua viwanda vya kuchakata mazao ili kuongeza thamani na soko la uhakika kwa wakulima. Sambamba na hilo, aliitaka Serikali kudhibiti bei za pembejeo na mazao ili wakulima wanufaike na jasho lao.
Mhe. Chomete amesisitiza pia kuwa hatua hizo zitachochea uzalishaji wenye tija, kuongeza kipato cha wakulima na kuimarisha uchumi wa Taifa.


