NA MASHAKA MHANDO, Tanga
MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Januari Makamba, ametoa wito kwa viongozi na wenye mamlaka nchini kutoa hukumu kwa haki, hekima na busara ili kulinda amani, umoja na mshikamano wa kijamii utakaorithishwa kwa vizazi vijavyo.
Makamba ambaye alikuwa mbunge wa Bumbuli na Waziri wa zamani, ametoa kauli hiyo Leo Machi 16 jijini hapa wakati akihutubia mamia ya wakazi wa Jiji la Tanga, viongozi wa dini, na wadau wa maendeleo katika hafla ya Iftar iliyoiandaa na marafiki zake wa jiji hilo kwenye Hoteli ya Tanga Beach Resort.
Katika hotuba yake iliyojaa hisia, Makamba amesisitiza kuwa mshikamano ulioonyeshwa na wananchi waliojitokeza kwa wingi ni kielelezo cha "urithi wa Tanga ya zamani" inayozingatia upendo, kutembeleana na kushirikiana bila kujali tofauti zao.
"Mmenipa heshima kubwa sana. Huu ni utamaduni wetu watu wa Tanga wa kupendana na kushirikiana. Ombi langu kwa walimu na masheikh ni dua; tuiombee nchi yetu na viongozi wetu, lakini kikubwa watu wenye mamlaka ya kuhukumu, wahukumu kwa haki na hekima ili jamii yetu ibaki kuwa na umoja," alisema Makamba.
Aidha, Makamba aligusia ziara yake katika taasisi za dini (Madrasa) aliyoifanya Machi 15, akiahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za walimu wa dini katika kuboresha mazingira ya elimu kwa watoto licha ya changamoto za miundombinu zinazozikabili taasisi hizo.
Kwa upande wake, mmoja wa waandaaji wa karamu hiyo, Salim Bawazir, aliwashukuru wananchi kwa kuitikia wito huo kwa wingi, akibainisha kuwa mahudhurio hayo yameonyesha upendo wa dhati kwa Makamba licha ya kuwepo kwa hafla nyingine ya Iftar mkoani hapa siku hiyo hiyo.
Bawaziri aliandaa na wenzake, Omari Mwasingo, Diwani wa kata ya Majengo Salimu Perembo na Akida Machai.
Baadhi ya washiriki wa hafla hiyo walieleza kutoridhishwa kwao na kitendo cha kuratibiwa kwa Iftar mbili kubwa kwa wakati mmoja ndani ya jiji la Tanga, wakieleza kuwa hatua hiyo inahatarisha kuwagawa waumini katika kipindi kinachohitaji umoja zaidi.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mashuhuri akiwemo Mkurugenzi Mstaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS), Rashid Othman, aliyekuwa mbunge wa Tanga Mjini, Ummy Mwalimu, viongozi wa taasisi za dini, madiwani na viongozi wa CCM mkoa na wilaya.











