Serikali yawataka vijana kuchangamkia fursa za mikopo

GEORGE MARATO TV
0


Na Mashaka Mhando, Muheza 

SERIKALI imetangaza mkakati wa kuhakikisha fursa za mikopo na zabuni za manunuzi ya umma zinawafikia vijana katika maeneo yote ya nchi ili kuwajengea uwezo wa kiuchumi na kupunguza ukosefu wa ajira.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Maendeleo ya Vijana), Joel Nanauka, ametoa kauli hiyo jana wilayani Muheza wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii ilipotembelea na kukagua shughuli za Kikundi cha Vijana cha ‘Mali Hai’.

Nanauka ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Muheza kuhakikisha inatenga asilimia 30 ya manunuzi ya umma kwa ajili ya vijana, ikiwa ni pamoja na kuwapatia zabuni za ujenzi kikundi hicho ambacho kimeonesha uaminifu kwa kurejesha mkopo wa Shilingi Milioni 20.

“Wizara itahakikisha vijana wanafikiwa kila kona ya nchi ili wanufaike na fursa hizi. Niwaombe vijana kutumia vyema Shilingi Bilioni 200 zilizotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya uwezeshaji wananchi,” amesema Nanauka.

Pia Waziri Nanauka amewataka vijana nchini kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa kupitia halmashauri ili kuanzisha miradi ya uzalishaji itakayowasaidia kujitegemea kiuchumi.

Waziri Nanauka amebainisha kuwa kikundi hicho ni mfano wa mafanikio ya uwezeshaji wananchi, ambapo tangu kilipopata mkopo wa halmashauri mwaka 2018, kimefanikiwa kukuza mtaji wake kutoka kiwango kidogo hadi kufikia zaidi ya Shilingi Milioni 52 hivi sasa.

“Hii ni sehemu ya mafanikio makubwa. Tunataka tuwawezeshe vijana wengi zaidi, hivyo niwaombe wachangamkie fursa hizi za mikopo ili waweze kuongeza mitaji na kujiendeleza,” amesema Nanauka.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Bunge, Hawa Chakoma, amesema wameridhishwa na maendeleo ya mradi huo na kuitaka Halmashauri ya Muheza kuendelea kukiwezesha kikundi hicho kwa kuongeza mitaji zaidi ili kikuze fursa za ajira kwa vijana wengine.

Pia amekipongeza kikundi hicho kwa nidhamu ya kurejesha mkopo na kuitaka Serikali kuendelea kuwapa kipaumbele katika mikopo mingine mikubwa zaidi.

Naye mjumbe wa kamati hiyo, Kange Lugola, ameshauri uongozi wa mkoa na halmashauri kutenga eneo kubwa zaidi la uwekezaji kwa ajili ya kikundi hicho, akieleza kuwa eneo lililopo sasa limekuwa dogo kulingana na kasi ya uzalishaji inayofanywa na vijana hao.

Awali akisoma risala ya kikundi hicho, Clara Godfrey amesema licha ya kufanikiwa kuajiri vijana 20 katika ufyatuaji matofali na ujenzi wa makaravati, bado wanakabiliwa na changamoto ya udogo wa eneo la uzalishaji na ukosefu wa vifaa kama gari la kusafirishia malighafi na mashine ya kisasa (mixer).

Kuhusu changamoto hizo, Waziri Nanauka amesema Serikali ya Mkoa wa Tanga kwa kushirikiana na Halmashauri ya Muheza itashughulikia urasimishaji wa eneo la kufanyia kazi kwa ajili ya kikundi hicho ili kuongeza ufanisi.

Kikundi cha Mali Hai kinajishughulisha na utengenezaji wa matofali, beacon, na utunzaji wa mazingira, kikiwa kielelezo cha mafanikio ya uwezeshaji vijana mkoani Tanga.






Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top