Na Mwandishi wetu Jovina Massano;Musoma
MKUU wa mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi amesema kuwa kukamilika kwa hospitali ya kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere iliyopo Kata ya Kwangwa Manispaa ya Musoma kutaimarisha Diplomasia tiba kwa nchi jirani.
Kanali Mtambi ameyasema hayo Machi 4,2026 wakati akizindua kambi ya matibabu katika hospitali hiyo inayosimamiwa na madaktari bingwa kutoka taasisi ya tiba ya mifupa na ubongo Muhimbili(Moi) ikionhozwa na Mkurugenzi Mtendaji Mh. Balozi ,Dkt Mpoki Ulisubisya.
Amesema kuwa ni miaka 3 tangu hospitali hii ianze kutoa huduma imeweza kupokea wagonjwa zaidi ya 200 kutoka nchi jirani kupata huduma za kitabibu katika hospitali hii ya kumbukumbu ya Mwl.Nyerere.
" Ujenzi wa hospitali hii utakapokamilika utaboresha mahusiano mazuri na nchi jirani kwa kuwa wale watakaofika na kupata huduma za matibabu hapa watakuwa mabalozi wema wa nchi yetu katika nchi zao", amesema Mtambi.
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya tiba ya mifupa na ubongo Muhimbili ( Moi) Balozi Dkt Mpoki Ulisubisya amesema hivi sasa taasisi ya MOI imeanza kutoa matibabu ya upasuaji kwa kutumia akili unde na kuacha kufanya upasuaji kihistoria ilivyokuwa hapo awali.
Amesema kuwa hivi taasisi inatoa huduma za kitabibu za kisasa kama vinavyotolewa kama maeneo mengine duniani, sasa ombi la kuendelea kubaki hapa limepokelewa kuja na mpango wa kuweka tawi la taasisi katika hospitali hiyo na kwa kuanza ndio maana wamefika kutoa huduma katika mkoa.
"Sisi tumepata fursa ya kuaminiwa na wananchi wa Tanzania na tunataka tuwaahidi kupitia katika hadhira hii kwamba hatuta waangusha kwa kuwa timu katika taasisi hii ipo chonjo kuendelea kutoa huduma za kisasa kama zinavyotolewa kwingine kote duniani", amesema Mpoki.
Aidha amesema kuwa mpaka sasa wamekwisha hudumia wagonjwa wapatao 231 katika hao wagonjwa 10 wamefanyiwa upasuaji katika hospitali hii,kama taasisi wameweza kuja na vifaa vitakavyotumika katika afua za kusaidia wagonjwa wenye mivunjiko mibaya ya mifupa,umri mkubwa na maumbile kwa kuja na vipandikizi.
Pia amemshukuru Mbunge wa viti Maalum Agnes Marwa alivyofika katika taasisi hiyo na kushuhudia huduma zinazotolewa na taasisi kwa niaba ya wagonjwa na wananchi.
Amewaeleza wananchi wote kuwa hivi sasa taasisi ya MOI inatibu asilimia 99 ya changamoto za mifupa na asilimia 97 hadi 98 za mfumo wa fahamu kwa njia za kisasa zinazotolewa katika maeneo mengine hapa duniani.
Kambi hiyo ya madaktari bingwa itatoa huduma mpaka Machi 7,2026 wananchi walio na changamoto za mifupa na Mfumo wa fahamu wafike kupata matibabu.
Kwa Upande wake Mbunge wa viti Maalum Agnes Marwa ameishukuru taasisi ya MOI kufika na kutoa tiba kwa wananchi wa mkoa huu na mikoa jirani.
"Mimi nilipoona nimepata matibabu katika taasisi ya MOI,watu wengi wanaamini nje ya nchi kuna matibabu mazuri kuliko hapa kwetu dhana hiyo tuiondoe kwani taasisi hii inafanya kazi vizuri sana kama zinazopatikana nchi za wenzetu, kutokana na huduma nzuri niliyoipata niliwiwa kuiomba taasisi kufika pia mkoani hapa na hatimaye Serikali nayo ikawa tayari na sasa wananchi wamekutana na madaktari bingwa na kuhudumiwa", amesema Agnes.
Serikali ya awamu ya sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Afya katika vipaumbele vyake kuhakikisha huduma za afya zinaboreshwa imeendelea kuimarisha huduma za matibabu ya ubingwa bobezi na tiba utalii kwa kuendeleza na kusimamia afua za tiba asili na tiba mbadala nchini wameweka utaratibu wa uendelezaji wa wataalam katika sekta ya Afya kwa fani za kati,ubingwa na ubingwa bobezi.
Nae Mwenyekiti wa CCM mkoa Mh.Patrick Chandi amesema siku mia za mh.Rais zimeonekana kwa vitendo huku akiwapongeza madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo kwa uwajibikaji pia ukamilikaji wake utakuwa umeisaidia wananchi wa Kanda ya Ziwa kupata huduma katika hospitali ya Serikali.
Uzinduzi huo umeshuhudiwa na mkuu wa Wilaya ya Musoma Juma Chikoka wananchi na viongozi wa chama na Serikali.







