Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Bara, Stephen Wasira, amesema mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi nchini hayawezi kufanikiwa kwa juhudi za Serikali pekee, bali yanahitaji ushiriki wa wananchi na wadau wote wa maendeleo, wakiwamo vyama vya siasa.
Akizungumza Februari 5, 2026, mjini Bunda Mkoani mara wakati wa maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa CCM, Wasira amesema rushwa bado ni changamoto kubwa inayokwamisha jitihada za maendeleo na kudhoofisha haki za wananchi.
Amesema kila Mtanzania ana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika vita dhidi ya vitendo hivyo kwa kutoa taarifa pale anapobaini rushwa, badala ya kulalamika bila kuchukua hatua.
“Rushwa ni siri kati ya pande mbili, anayetoa na anayepokea. Mamlaka haziwezi kujua kinachoendelea bila ushirikiano wa wananchi,” amesema Wasira.
Aidha,amefafanua kuwa hata pale mtu anapolazimika kutoa rushwa ili kujiokoa, hapaswi kuishia hapo bali awasilishe taarifa kwenye mamlaka husika ili wahusika wachukuliwe hatua.
Katika maelezo yake, Wasira amesema CCM inaendelea kuonesha msimamo wa kupinga rushwa kwa vitendo kupitia ilani na misingi ya chama, akisisitiza kuwa rushwa ni dhuluma inayonyima wananchi maendeleo yao ya haki.
Amegusia pia mjadala ulioibuka baada ya baadhi ya wabunge kuitwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), akisema hatua hiyo haikulenga kuwatisha bali ilikuwa ni sehemu ya kukusanya taarifa kwa ajili ya uchunguzi.
“Takukuru haina nia mbaya. Wanataka taarifa za kina ili wachukue hatua stahiki. Hili liwe funzo kwa Watanzania wote kutoa taarifa wanapokutana na changamoto hizo,” amesema.
Akizungumzia masuala ya haki na amani, Wasira amesema mambo hayo hayawezi kutenganishwa, akifananisha uhusiano wake na kuku na yai. Amesema pasipo amani, haki haiwezi kupatikana, akitolea mfano maeneo yenye migogoro kama Gaza na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Amesema CCM imejipambanua kama chama kinacholinda amani kwa sababu kinaamini kuwa msingi wa haki na maendeleo ni uwepo wa amani ya kudumu.
Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu, “Tumechagua amani na umoja kwa maendeleo yetu,” amesema ni mwendelezo wa dhamira ya muda mrefu ya chama ya kujenga taifa lenye mshikamano, haki na maendeleo.



