....Ni sehemu ya kumbukizi ya miaka 27 ya kifo cha Profesa Hubert Kairuki
Na Mwandishi Wetu
ZAIDI ya wananchi 500 wamepatiwa huduma ya uchunguzi wa maradhi mbalimbali na ushauri wa bure katika siku ya kwanza ya kambi hiyo katika hospitali ya Kairuki iliyoko Mikocheni jijini Dar es Salaam.
Naibu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Dk Muganyizi Kairuki amesema leo kuwa wameamua kutoa huduma hizo bure kama sehemu ya kumuenzi mwasisi wa hospitali hiyo, Hayati Profesa Hubert Kairuki aliyefariki miaka 27 iliyopita.
Alisema huduma hiyo ya uchunguzi inafanyika katika hospitali hiyo na kituo chao cha matibabu kilichoko katika Kituo cha Mabasi cha Magufuli Mbezi jijini Dar es Salaam.
Dk Muganyizi alitaja baadhi ya huduma zinazotolewa kwenye kambi hiyo kuwa ni pamoja na uchunguzi wa uvimbe katika tezi dume, uzimbe katika kizazi, uvimbe kwenye uvimbe kwenye matiti.
Alisema katika siku ya kwanza pekee idadi ya waliojitokeza imekuwa kubwa kupita kawaida lakini walifanikiwa kuwafanyia uchunguzi na kuwapa ushauri zaidi ya wananchi 500 waliojitokeza.
“Kwa kweli idadi ya wananchi ambao wamejitokeza ni kubwa sana na tunatarajia kambi hii itaendelea kwa siku zingine tatu kwa hiyo wananchi ambao hatujawafanyia uchunguzi leo (Jumatatu) bado wana siku zingine za kuja kupata huduma hapa,” alisema Dk Muganyizi
Dk Muganyizi alisema kuelekea maadhimisho hayo ya miaka 27 ya kumbukizi ya mwasisi wa hospitali hiyo pia watakuwa na mhadhara wa kisayansi siku ya Alhamisi wiki hii.
Aidha, alisema pia wanatarajia pia kuzindua mtambo wa kisasa wa kuongeza mafanikio katika upandikizaji mimba ambao unatoa uhakika wa upandikizaji mimba kiitwacho Lasser.
“Kwenye upandikizaji mimba zamani ilikuwa mnafanya lakini mnategemea zaidi bahati lakini kifaa hiki kinachoitwa Lesser kinaondoa hali hiyo, kinaondoa hali ya kutegemea bahati katika upandikizaji mimba kwa sababu kinakupa majibu sahihi kwamba kinachofanyika kitazaa matunda au la,” alisema Dk Muganyizi
Alisema katika kumbukizi hiyo pia Kairuki Green IVF itaadhimisha miaka mitatu ya huduma tangu ilipofunguliwa rasmi ambapo mpaka sasa kimefanikiwa kupata watoto zaidi ya 140 kwa upandikizaji wa mimba.







