Benki ya Azania hii leo imezindua huduma mbili mpya zitakazonufaisha Wanafunzi wa
vyuo vya elimu ya juu pamoja na Watumishi wa Umma na wale wa sekta binafsi
zinazojulikana kama “Boom Advance” na “Salary Advance.”
Akizungumza katika uzinduzi huo, Ofisa Mwandamizi wa Masoko wa Benki hiyo Bi.
Elizabeth Nyattega alisema kuwa hatua hiyo ni muitikio wa mahitaji halisi ya wateja na
ni ukombozi mkubwa kwa Wanavyuo na wafanyakazi wa sekta ya umma na sekta
binafsi.
“Boom Advance” ni huduma inayowalenga Wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu
wanaopata mikopo kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) ambapo sasa
hawatalazimika kusubiri hadi mikopo yao iingie kwenye akaunti, bali wataweza kupata
mkopo wa muda wenye masharti nafuu ili kujikimu wakati wakisubiri fedha kutoka Bodi
ya mikopo”, alisema Nyattega huku akiongeza kuwa huduma ya “Salary Advance”
yenyewe ni mahsusi kwa Watumishi wa Umma au sekta binafsi ambapo kupitia huduma
hii mwajiriwa huyu ataweza kukopa sehemu ya mshahara wake kabla ya tarehe ya
kawaida ya mshahara wake kuingia. Kupitia mkopo huu wa muda mfupi, mwajiriwa
ataweza kukidhi mahitaji yake muhimu ya kifedha wakati akisubiri mshahara kuingia
mwisho wa mwezi. Mkopo hurudishwa pale mshahara unapoingia, kwa riba nafuu ya
5% tu na anaweza kukopa hadi nusu ya mshahara wake wa mwezi.
“Huduma hizi zote zinapatikana kwa urahisi kupitia simu yako ya mkononi kwa kubofya
*150*75#, kupitia Azania Bank Mobile App au Internet Banking”, alimalizia Nyattega.







