Na Mwandishi Wetu, Tanga
Serikali imesema uwekezaji uliofanyika katika Bandari ya Tanga unaenda kuleta nafasi kubwa kiuchumi Kitaifa na Kimataifa.
Hayo yamesemwa leo Septemba Mosi, 2025 na Msajili wa Hazina ( OTR) Nehemia Kyando Mchechu mara baada ya kufanya ziara ya kikazi katika bandari hiyo.
Akiongea mara baada ya kupokea taarifa ya utendajikazi wa bandari hiyo, Mchechu alisema kuwa uwekezaji uliofanywa na Serikali ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan uliogharimu kiasi cha shilingi za Kitanzania Bilioni 429.1 umefanya meli kubwa kuweza kutia nanga katika bandari hiyo.
“Uwekezaji huu ukianza na sehemu ya kutolea huduma yenye urefu wa mita 450, kina cha maji kutoka mita 3 kuwa mita 13, na lango la kuingilia kutaniliwa kufikia upana wa mita 135 lakini bado kuna mipango inayofanyika ya kuongeza tena mita 900”. Aliongeza Mchechu
Aidha Mchechu alisema kuwa,ukiangalia uwekezaji huu tunahakikisha kuwa sekta binafsi pamoja na sekta za umma zinaungana katika kufanya uwekezaji mkubwa chini kwa manufaa ya umma kwa ujumla.
Katika hatua nyingine Mchechu aliwapongeza wafanyakazi wa Bandari ya Tanga na aliwasihi waendelee kufanyakazi kwa bidii nakuiona bandari ni sehemu ambayo ni jicho la Serikali katika uchumi wa nchi.
“Lakini pia niwasihi wafanyakazi wa bandari hii tuone ufahari tupo sehemu ambayo ni jicho na mboni ya Serikali katika uchumi wa nchi hivyo lazima tuichukulie kama sehemu muhimu inayohitaji huduma zilizobora na tija kwa ajili ya maendeleo “. Alisema Mchechu
Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania Plasduce Mikaeli Mbossa alisema kuwa uwekezaji huo umesaidia kuhudumia meli kwa urahisi na gharama nafuu.
“Gharama za usafirishaji zinapokuwa nafuu zinasababisha yule ambaye ni mwekezaji wa viwanda anaweza kujenga viwanda mfano viwanda vya Simenti, viwanda vya katani ukuaji wake unatokana na kuimarika kwa miundombinu ya bandari”. Aliongeza Mbossa
Kwa upande wake Meneja wa Bandari ya Tanga Masoud Athumani Mrisha alimhakikishia Msajili huyo kuwa huduma katika Bandari ya Tanga itazidi kuimarika.
“Sisi wafanyakazi wa Bandari ya Tanga tunasisitiza huduma katika Bandari ya Tanga itazidi kuimarika kwa maana ya kwamba meli ikija tutaihudumiwa sio zaidi ya siku 3 meli inaondoka, hivyo alitoa wito kwa watumiaji wa bandari hiyo waendelee kuitumia bandari hiyo.









