Skip to main content

@marato_tv

@marato_tv
#sauti_ya_jamii

Kauli ya Rais Samia kuhusu kufurushwa kwa wanaharakati yagonganisha maafisa wakuu wa Serikali ya Kenya



 RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameibua mjadala nchini Kenya, kufuatia onyo lake kwa wanaharakati wa haki za binadamu kutoka Kenya na Uganda waliotimuliwa Tanzania kwa kuhudhuria kesi ya kiongozi wa upinzani, Tundu Lissu.

Huku waliotimuliwa wakiapa kushtaki serikali ya Tanzania, Waziri wa mashauri ya kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi ameonekana kugongana na katibu wake Korir Arap Sing’oei. 

Huku Mudavadi akiunga Rais Suluhu Dkt Sing’oei alihimiza Tanzania kuheshimu misingi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Akizungumza kwenye Citizen TV usiku wa Jumanne, Mudavadi alionekana kuunga mkono kauli za Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu kile alichokitaja kuwa ‘kuingilia masuala ya ndani’ ya Tanzania na kuonyesha wasiwasi wake kuhusu ‘ukosefu wa maadili’ wa Wakenya katika mienendo yao ya hivi karibuni.

Tofauti na Mudavadi,Katibu Sing’oei, aliitaka serikali ya Tanzania kuwaachilia mara moja Jaji Mkuu Mstaafu Willy Mutunga na ujumbe wake,

Sing’oei alisisitiza kuwa kuzuiliwa kwa ujumbe huo wa Kenya kulikiuka misingi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), ambayo inahimiza uhuru wa kusafiri, na ushirikiano kati ya nchi wanachama.

“Tunasihi serikali ya Tanzania kuachilia aliyekuwa Jaji Mkuu wa Kenya na ujumbe wake, kwa mujibu wa taratibu na misingi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki,” alisema Sing’Oei.

Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna alishangaa jinsi waziri Mudavadi anaweza kuunga kutimuliwa kwa Wakenya kutoka nchi mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Bw Sifuna alitilia shaka msimamo wa Mudavadi kuhusu haki za Wakenya nje ya nchi.

Kulingana na Sifuna, ni jambo la kushangaza kwa Waziri huyo kutoa matamshi hayo ilhali Wakenya, akiwemo mwanaharakati na mwandishi wa habari Boniface Mwangi, aliokamatwa nchini Tanzania hajulikani aliko.

‘Kwa Waziri wetu wa Masuala ya Nje kuunga mkono Tanzania kuhusu kufukuzwa kwa Wakenya ni jambo la ajabu. Ni nani aliwaweka hawa watu madarakani? Hawana maana kabisa,’ Sifuna alilalamika.

Kulingana na Mudavadi, Rais Suluhu huenda alizungumza kwa kuzingatia tabia za baadhi ya Wakenya hivi karibuni.

‘Sitapinga kauli hiyo (ya Suluhu) kwa sababu nafikiri kuna ukweli fulani. Tuwe wakweli. Kiwango cha lugha chafu na matusi tunayoona Kenya, ingawa tuna uhuru wa kujieleza, wakati mwingine kinavuka mipaka. Anasema watu wamekuwa wakivuka mipaka katika kauli zao, jambo ambalo ni la kweli,’ alisema Mudavadi.

Mnamo Jumapili, kiongozi wa chama cha Peoples Liberation Party, Martha Karua, alizuiwa kuingia Tanzania akiandamana na watetezi wa haki za binadamu na wanasheria, Lynn Ngugi na Gloria Kimani.

Karua alisema alifukuzwa nchini humo baada ya kuzuiliwa kwa muda mrefu katika uwanja huo wa ndege.

Siku moja baadaye, wanaharakati wengine watatu wa Kenya, akiwemo Jaji Mkuu wa zamani Willy Mutunga, walikamatwa.

Mutunga, aliyekuwa akisafiri na mwanaharakati Hanifa Adan pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa VOCAL Africa, Hussein Khalid, alikamatwa walipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere baaada ya kurejeshwa Kenya.

Jana, Bw Khalid alisema mwanaharakati maarufu Boniface Mwangi kutoka Kenya, pamoja na mwandishi na wakili kutoka Uganda, Agatha Atuhaire, waliokamatwa na maafisa wa Tanzania hawajulikani waliko.

“Boniface Mwangi na Agatha Atuhaire hawajulikani walipo. Baada ya kutumia njia zote jijini Dar es Salaam, hatujaweza kuthibitisha waliko. Tumekagua mashirika yote ya ndege na tumefuatilia kwa wanasheria nchini Tanzania, lakini bado hawajulikani waliko,”alisema Khalid.

“Tumejaribu kuwatafuta pamoja na watetezi wa haki za binadamu na wanasheria nchini Tanzania bila mafanikio. Ijulikane kuwa Wakenya watamlaumu Rais Suluhu Hassan binafsi endapo chochote kitatokea kwa wawili hao.”

Mnamo Jumanne, Boniface Mwabukusi, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), alitangaza kuwa serikali ya Tanzania ilimtimua Mwangi na Atuhaire.

Katika taarifa yake, Mwabukusi alisema wawili hao walifukuzwa chini ya usimamizi wa maafisa wa uhamiaji wa Tanzania.

“Boniface Mwangi, mwandishi wa habari na mwanaharakati wa haki za binadamu kutoka Kenya, na Bi Agatha Atuhaire, mwandishi wa habari na wakili kutoka Uganda, ambao walikuwa wakizuiliwa katika Kituo cha Polisi jijini Dar es Salaam, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tangu Mei 19 2025, wamefukuzwa na kurejeshwa katika nchi zao,” alisema Mwabukusi.

Mwangi, aliyewasili Tanzania Jumapili kuhudhuria kesi ya kiongozi wa upinzani Tundu Lissu iliyopangwa siku iliyofuata, alikamatwa siku ya Jumatatu, Mei 19, baada ya serikali ya Tanzania kudai aliingia nchini humo kwa njia isiyo halali.

Comments

#maratotv

RAIS RUTTO AAMBATANA NA ODINGA NCHINI CHINA

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mh William Rutto na mke wake wamewasili nchini China kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi na Serikali wa Jukwaa la ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC). Katika ziara hiyo ameambatana na waziri mkuu mstaafu wa nchi hiyo Raila Odinga ambaye pia anapigiwa kampeni ili aweze kushinda nafasi ya Uenyekiti wa AU.

WIZARA YA MALI ASILI YASISITIZA MATUMIZI YA SHERIA NA KANUNI KATIKA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA UHIFADHI

Na.Joyce Ndunguru, Morogoro. Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii anaeshughulikia Maliasili, Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba asisitiza matumizi ya sheria na kanuni katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za uhifadhi. Kamishna Wakulyamba ameyasema hayo leo Septemba 1, 2024 wakati wa ziara ya kikazi aliyoifanya katika ofisi za Makao Makuu ya TAWA yaliyopo Mkoani Morogoro kwa lengo la kuongea na watumishi ili kuimarisha utendaji kazi pamoja na kukagua maeneo ya kazi. "Kama wahifadhi tunapaswa kufahamu sheria zote zinazosimamia masuala ya uhifadhi zilizopo katika Taasisi zetu pamoja na za Taasisi zingine za uhifadhi zilizopo ndani ya Wizara ya Maliasili na utalii" amesema Kamishna Wakulyamba. "Pamoja na kufahamu sheria na kanuni zilizopo ndani ya Wizara yetu, ni vyema kufahamu na kuzingatia sheria nyingine za Nchi ambazo zinatuzunguka ili ziweze kutusaidia katika utekelezaji wa majukumu yetu mfano sheria inayohusiana na ukusanyaji wa vielelezo kuanzia kw...

Rais Dkt. Samia Awasili China Kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano Kati ya China na Africa FOCAC

  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Beijing Capital nchini China kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) tarehe 03 Septemba, 2024.

Wananchi Serengeti Wamtaja Dkt Rhimo Nyansaho Kama Chachu ya Maendeleo Kwao

Na Shomari Binda-GMTV  WANANCHI Wilaya ya Serengeti mkoani Mara wamemtaja Dkt.Rhimo Nyansaho kama chachu ya maendeleo kupitia taasisi yake ya Nyansaho Foundation. Wakizungumza kwa nyakati tofauti na GMTV wananchi hao wamesema kwa kipindi kirefu mchango wake umeonekana katika kuisaidia jamii. Wamesema ukifika Jimbo la Serengeti kila Kata na Kijiji huwezi kukosa mkono wa Dkt.Nyansaho kuchangia na kusaidia jamii kuanzia elimu,afya,maji na masuala mengine ya jamii. Mmoja wa wananchi hao aliyejitambulisha kwa jina la Mwita Sagati amesema wapo watu wanaojitokeza kusaidia jamii kipindi cha uchaguzi kwa kulenga kupata uongozi lakini imekuwa tofauti kwa Dkt.Nyansaho. Sagati amesema iwapo atajitokeza kuomba nafasi ya ubunge wapo tayari kumpambania na kumchagua ili aweze kuendelea kutoa mchango wake katika kusaidia jamii. " Tunashukuru sana mchango wa Dkt.Nyansaho kwa kuchangia shughuli za maendeleo hapa Serengeti. " Wengine huwa wanakuja nyakati za uchaguzi lakini huyu mchango wake ni ...

MAKOMANDOO MIAKA 60 YA JWTZ,HAIJAWAHI KUTOKEA

Makomandoo ya jeshi la ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ)wamekuwa kivutio cha aina yake kwenye kikele cha maadhimisho ya miaka 60 ya tangu kuanzishwa kwa jeshi hilo. Katika sherehe hizo ambazo zimefanyika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshiriki kwenye kilele cha Maadhimisho ya Miaka 60 ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika uwanja huo wa Uhuru Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 1 Septemba, 2024. Rais ameonesha kujivunia na kulipongeza JWTZ kwa kufanya kazi kwa kufuata misingi ya kuanzishwa kwake huku akitumia nafasi hiyo kuwapongeza Marais waliomtangulia kwa kazi kubwa waliyofanya wakati wa uongozi wao kwa kuliongoza vema jeshi hilo.

Meli ya Mv. Serengeti yapinduka na kuzama katika Bandari ya Mwanza kusini

 Meli Mv.Serengeti imepinduka na kuzama kwenye bandari ya mwanza kusini.  Meli hiyo imepinduka na kuzama disemba 26 majira ya saa Saba za usiku.  Tukio hilo limetokea meli hiyo ikiwa imefungwa katika gati la bandari ya mwanza kusini.  Kampuni ya meli Tanzania(Tashico) imethibitisha meli ya Mv. Serengeti kupinduka na kuzama upande mmoja wa nyuma.  Kwa Mujibu wa Taarifa iliyotolewa na kitengo cha Masoko na Uhusiano kwa Umma cha Kampuni hiyo inaeleza kuwa Tashico imeshirikiana na Timu mbalimbali za Wataalam kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania(TASAC), Mamlaka ya Usimamizi wa bandari (TPA) na wadau wengine katika Juhudi za Uokoaji.  Kwa Mujibu wa Taarifa hiyo,Taarifa rasmi ya chanzo cha Tatizo itatolewa Meli hiyo itakapokuwa imeinuliwa na Uchunguzi wa kubaini Tatizo utakapokuwa umefanyika. Meli ya Mv.Serengeti inadaiwa kusitisha safari zake kwenye ziwa Victoria mwaka 2016  Meli ya Mv.Serengeti imepinduka na kuzama katika...

Mbunge wa Bukoba Vijijini ameaga Sifa Kedekede Kwa Rais Samia

 Na Angela Sebastian; Bukoba  MBUNGE wa jimbo la Bukoba vijijini Dk. Jasson Rweikiza amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya wananchi wa jimbo hilo, kwa kuwapatia zaidi ya shilingi bilioni 19 kwa ajili ya ujenzi wa madaraja mawili ambayo ni lango la kutoka na kuingia ndani ya mkoa wa Kagera. Ametoa shukrani hizo wakati akiongea wananchi mbalimbali waliofika katika viwanja vya Rweikiza pre and Primary school iliyoko eneo la Kyetema Bukoba vijijini, kwa kwa ajili ya kumbukizi ya miaka 100 ya kuzaliwa baba wa mbunge huyo aliyekuwa akiitwa Samsoni Rweikiza.  Rweikiza amebainisha kuwa,Dk. Samia Suluhu Hassan ni Rais mwenye upendo amekubali kutoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya Bukoba Vijijini na ndiyo maana tunasema atakuwa kiongozi wetu kwa awamu nyingine tena,tunapaswa kila mmoja kumuunga mkono. ametaja madaraja hayo kuwa ni Karebe ambalo limetengewa kiasi cha shilingi bil.9.3 kwa ajili ya ukarabati mkubwa kutokana na daraja ...

Jenerali Jacob Mkunda Atembelea Meli Tiba ya China Aridhishwa na Huduma

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob John Mkunda ametembelea meli tiba ya Jeshi la Ukombozi la Watu wa China Peace Ark ili kuona matibabu yanavyofanyika. Jenerali Mkunda amefurahishwa na namna wataalam wa tiba wa Jeshi la China walivyotoa matibabu kwa kushirikiana na wataalam wa tiba wa JWTZ . Meli tiba ya jeshi la China imekuja hapa nchini na kutia nanga kwenye bandari ya Dar Es Salaam kutoa matibabu mbalimbali kwa wananchi ikiwa ni muendelezo wa maadhimisho ya miaka 60 tangu kuanzishwa kwa JWTZ  na ushirikiano wa miaka 60 baina ya JWTZ na Jeshi la Ukombozi la Watu wa  China. Matibabu hayo yalianza kutolewa tarehe 18 Julai 2024 hadi tarehe 22 Julai 2024. Meli tiba hiyo itaondoka hapa nchini tarehe 23 Julai mwaka huu.

AMIRI JESHI MKUU AKAGUA GWARIDE LA MIAKA 60 YA JWTZ

 Mapema leo asubuhi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Mhe.Dkt,Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride Maalumu la Maadhimisho ya Miaka 60 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Uwanja wa Uhuru leo September 01,2024. Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza kuwa jeshi la ulinzi la Wananchi Tanzania si jeshi la Uvamizi bali ni jeshi la ulinzi wa Wananchi Tanzania Amewahakikishia wanajeshi kufanya kazi kifua mbele,kuwa amiri jeshi mkuu yuko pamoja nao wakati wote.

Jenerali ameacha alama ya uzalendo na kujitoa kwa ajili ya Taifa

*📌 Serikali itaenzi na kuthamini mchango wake* *📌 Asema Jenerali Musuguri alijitolea kuhakikisha Tanzania inabaki na amani na usalama* *📌 Asema alikuwa mstari wa mbele kuliokoa Taifa* *📌 Aiasa jamii kuacha alama katika maisha ya kila siku* *📌 Dkt. Biteko aongoza mamia ya watu mazishi ya Jenerali Musuguri Butiama* Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa  aliyewahi kuwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Mstaafu David Bugozi Musuguri alijitolea  kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa na amani, usalama na mshikamano pamoja na kuifundisha jamii  moyo wa dhati wa kuilinda nchi. Dkt. Biteko amesema hayo leo Novemba 4, 2024 Butiama mkoani Mara wakati akiwasilisha salamu za Serikali kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mazishi ya Jenerali Mstaafu Musuguri. “ Katika  uhai wa kila mmoja wetu ni jambo gani mtu atakumbukwa nalo, baba huyu a...