Meneja wa Shirika la Ndege na Vituko Hivi....

GEORGE MARATO TV
0


MOJAWAPO ya makosa yaliyowahi kutendwa na mashirika ya ndege barani Afrika, ni tukio la mwaka 1988 ambapo Meneja Mkuu wa Shirika la Ndege la Uganda aliachwa na ndege ya abiria na akaamuru irejee uwanjani kumchukua.

Meneja huyo alichelewa kufika uwanjani hapo tayari kusafiri kwa ndege hiyo, na ndipo aliwaamuru waongoza ndege kuwaambia marubani kurejesha ndege hiyo aina ya Boeing 747 - Jumbo Jet.

Ni katika utawala huu wa Rais Yoweri Museveni ambapo meneja huyo alivurugwa na kutoa amri hiyo ya ajabu, ambayo pia ilimharibia kazi yake siku hiyo hiyo.

Wakati huo shirika la ndege la Uganda lilikuwa limekodisha ndege za shirika la ndege la Uholanzi, KLM, kwa ajili ya safari za nje ya Uganda.

Katika tukio hilo, ndege hiyo ikiwa na abiria iliondoka uwanja wa ndege wa Entebbe saa 2 asubuhi kwenda Bombay nchini India.

Ndege ikiwa inaondoka uwanjani hapo ndipo maneja huyo ambaye alitakiwa asafiri nayo kwenda kwenye mkutano nchini India, aliwasili uwanjani hapo akiwa amechelewa na kuachwa.

Meneja huyo kwa haraka alipanda ngazi mpaka juu katika chumba cha kuongoza ndege na kuwaamuru waongoza ndege kuwaambia marubani wa ndege hiyo warejee uwanjani hapo ili kumchukua.

Waongoza ndege waligoma na kusema tayari ndege ipo safarini angani ikiwa imejaza mafuta mengi kwa safari hiyo ndefu, na kwamba bado ni nzito kuweza kurejea na kutua.

Huku wakiwa na mshangao, waongozaji hao walimwambia meneja huyo kwamba wao hawatawaambia marubani kuvunja safari bila kuwepo dharura yoyote.

Hata hivyo, meneja huyo alisisitiza akisema kuwa ni lazima asafiri siku hiyo, kwa kuwa safari yake ya India ina ujumbe wa kutoka kwa Rais Museveni kwenda kwa serikali ya India.

Aliwaambia waongozaji hao wamuunganishe na marubani wa ndege hiyo ili awaamuru warejee uwanjani Entebbe.

Wakati malumbano hayo yakiendelea hapo ndani ya chumba katika mnara wa kuongoza ndege, zilisikika sauti za marubani wa ndege hiyo wakitoa miito kwa uwanja wa ndege wa Addis Ababa, Ethiopia, na uwanja wa ndege wa Nairobi, Kenya, kuwaarifu kuwa ndege yao itapita katika anga ya nchi hizo ikiwa safarini kwenda Bombay.

Hapohapo ndipo pia marubani hao Wazungu walipopokea simu kutoka Entebbe, na wakashangaa kuambiwa kuwa warejee uwanjani kumchukua bosi wao.

Meneja huyo aliwatisha marubani hao kwamba yeye ametumwa na Rais Museveni kwenda India, na kwamba wasiporejea Entebbe wajiandaa kupoteza kazi.

Na kumbuka wakati huo Museveni alikuwa katika mwaka wa pili wa utawala wake wa kijeshi nchini Uganda, na alikuwa mkali kwa kila nyanja.

Hatimaye marubani hao walitii na kuwatangazia abiria kwamba ndege yao inarejea Entebbe kwa sababu ya dharura ya kawaida (sio kwa dharura hatarishi).

Ndege ilivunja safari hiyo na kurejea, lakini kabla ya kutua Entebbe rubani walitoa sharti moja kwamba lazima ndege hiyo imwage robo 3 ya mafuta yake kwenye Ziwa Victoria ili iwe nyepesi kuweza kutua uwanjani.

Maneja huyo alipoambiwa atoe idhini ya kumwagwa mafuta ziwani, na alisema OK.

Ndege ilipotua, marubani hao na wafanyakazi wote 12 wa ndege hiyo walikwenda moja kwa moja ofisini kwa Meneja Mkuu huyo kumkabili na kuhoji kulikoni.

Baada ya malumbano makali ofisini hapo, marubani hao waligoma kuanza tena safari hiyo ya Bombay na kusema kuwa tayari wamemaliza kazi yao siku hiyo, na wakaondoka kurejea hotelini kwao, huku pia wakitoa kashfa nyingi dhidi ya Afrika.

Kwa upande wa abiria, shirika hilo la ndege la Uganda ililazimika kuingia gharama nyingine kuwaunganisha abiria hao kwenye ndege za mashirika mengine ili waendelee na safari yao ya Bombay.

Aidha kama ilivyotarajiwa, baadaye taarifa ya tukio hilo ilimfikia Rais Museveni, ambapo meneja huyo alifukuzwa kazi siku hiyo hiyo bila kuundiwa tume ya kuchunguza tukio hilo.

Tukio hilo lililaaniwa na mno nchini Uganda, ambapo pia jarida la the "NewAFRICAN" liliandika kwa kina habari hii ya tukio hilo.

PICHA: Boeing 747 ya KLM, ikipita jirani na mnara wa kuongozea ndege.




 

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top