📍 Asema nadhiri aliyoweka ilitokana na watoto kusoma umbali mrefu
📍 Asema alipokosa fedha serikali alianzisha msalagambo kusaka marafiki zake kutimiza nadhiri yake
📍 Awashukuru CRDB Benki, Karimjee Foundation kumsaidia kujenga madarasa mawili na vyoo
📍 CRBD yaungana na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kumpongeza MwanaFA kwa kazi nzuri anayofanya Muheza
📍 Mtendaji wa Kijiji Ataka umbali waliokuwa wakisoma watoto wa Kijiji cha Misufini
📍 Wazazi Misufini Wasema hawakukosea kumchagua MwanaFA kuwa mbunge, wamtaja pia Rais
Na Mwandishi Wetu, Magoroto
NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Hamisi Mwinjuma maarufu MwanaFA, alisema alijiapiza na kuweka nadhiri ya kujenga shule ya msingi katika Kijiji cha Misufini kilichopo kata ya Magoroto kilichokuwa kikikabiliwa na changamoto lukuki.
Sambamba na nadhiri hiyo, MwanaFA hakutegemea kama wananchi wa Kijiji hicho wangekichagua Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwakuwa walikabiliwa na changamoto nyingi.
Alisema Kijiji hicho kilikuwa kikikabiliwa na tatizo la ukosefu wa Maji, Umeme, shule na barabara ambazo sasa tangu awe mbunge, huduma zote hizo amewafikishia.
Akizungumza katika hafla ya kukabidhiwa shule shikizi iliyojengwa na wahisani wake, Benki ya CRDB Machi 26 2025, MwanaFA alisema alijua matatizo hayo alipokwenda kufanya kampeni kuomba kura za Rais, Diwani na Mbunge mwaka 2020.
Alisema alifika katika Kijiji hicho Septemba mwaka 2020 kuomba kura akiwa na wenzake, lakini walilazimika kuacha magari katika Kijiji cha Gare kutokana na Kijiji hicho kukosa barabara ya kufika makao makuu ya Kijiji hicho.
Alisema alipofika katika Kijiji hicho walifanya mkutano na kundi la watoto wa shule waliwasindikiza kurudi Gare huku wakiwaambia nyimbo mbalimbali.
Alisema wale watoto aliwauliza "kwanini nyie hamchoki, wakasema wao Kila siku wanaenda na kurudi Gare kwenda kusoma.
Alisema kitendo cha watoto wale kuwasindikiza walitumia falsafa ya kumfikishia ujumbe kwamba wanauhitaji mkubwa wa kupata shule ili wasome karibu na nyumbani kwao.
"Kwahiyo Mimi nikajiapiza, nikaweka nadhiri ya kwamba moja ya mambo nitakayofanya ni kuwajengea shule wapate elimu yao hapa Kijijini kwao," alisema.
MwanaFA alisema baada ya kuchaguliwa aliulizia halmashauri kuona uwezekano wa kujenga shule katika Kijiji hicho lakini halmashauri hawakuwa na bajeti.
"Nikaamua kufanya msalagambo wa kuwatafuta marafiki zangu kuhakikisha shule hii inajengwa, nawashukuru ndugu zangu wa CRDB kwa kunisaidia kujenga madarasa mawili na matundu sita ya vyoo," alisema.
Alisema watu wengine waliomjengea madarasa mawili ni Richard Karimjee kupitia taasisi yake ya Karimjee Foundation nao pia aliwashukuru na yeye mwenyewe amejenga madarasa mawili. Jumla shule hiyo ina vyumba sita.
Mbunge huyo wa Muheza, alimwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya hiyo, Dkt Jumaa Mhina kuhakikisha anaipatia walimu shule hiyo ili watoto hao waweze kusoma jirani na Kijiji chao lakini pia kutengeneza barabara kutoka katika shule hiyo hadi Kijijini.
Akizungumza katika hafla hiyo Mjumbe wa bodi ya Wakurugenzi ya benki ya CRDB, Miranda Mpogolo alisema shule hiyo wameijenga kwa gharama ya shilingi milioni 66.1 kupitia sera yao ya kusaidia jamii.
Alisema kuwa benki hiyo imeandaa sera maalum ambayo inasaidia jamii katika miradi ya Elimu, Afya na mazingira ambapo kwa mwaka jana pekee walitumia zaidi ya shilingi bilioni 2.3 kusaidia miradi ya maendeleo ya jamii nchini.
Alisema walipopokea ombi la mbunge wa Muheza waliguswa sana na hata pale alipomwambia Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alipofanya ziara wilayani Muheza waliona umuhimu mkubwa wa kujenga shule hiyo.
"Tunakupongeza mhe mbunge kwa kazi nzuri unaiyofanya hapa Muheza, tumeona Rais akiwa Muheza kwenye ziara yake alikupongeza kwa kazi kubwa unayoifanya, na sisi CRDB benki ni mashuhuda na tunaungana naye kwa pongezi hizo, tunakupongeza sana," alisema Mpogolo.
Akisoma taarifa fupi Mtendaji wa Kijiji cha Misufini Pius Emanuel alimshukuru mbunge kwa kufanikisha upatikanaji wa shule hiyo akieleza kwamba umewasaidia watoto kuepukana na umbali mrefu wa kufuata shule.
Alisema watoto 100 walikuwa wakitembea umbali wa kilomita 12 kwenda na kurudi katika shule ya msingi Gare na wanafunzi wengine 60 walilazimika kutembea kilomita 14 kwenda na kurudi shule ya msingi Tongwe.
"Wanafunzi wengi waliacha shule kutokana na umbali huo, wasichana walikatisha ndoto zao hivyo hili ulilolifanya mheshimiwa mbunge ni jambo kubwa ambalo tunahitaji kukuunga mkono," alisema mtendaji huyo.
Katika risala ya wazazi iliyosomwa na wanafunzi walisema jambo ambalo mbunge huyo amelifanya kiukweli watamuunga mkono kutokana na ahadi zake kuwa za kweli.
"Sisi hatukukosea kukupa ubunge lakini pia Rais Dkt Samia Suluhu Hassan hajakosea kukuteua kuwa Naibu Waziri unastahili kwasababu ni kiongozi unayetatua changamoto zetu kwa uhakikika hongera sana," ilisema risala hiyo.




.jpg)











