Na Mashaka Mhando, Lushoto
ZAIDI ya wakazi 2,000 wa vijiji vya Mkundi-Mtae na Mkundi-Mbaru vilivyopo kata ya Mnazi tarafa ya Mtae, Jimbo la Mlalo wilayani Lushoto, watanufaika na mradi mkubwa wa Maji unaoendelea kutekelezwa na serikali.
Mradi huo wenye thamani ya sh. 787,204,963 unatekelezwa katika vijiji hivyo ambavyo vipo katika uwanda wa tambarare wilayani hapa na kwa muda mrefu vilikuwa vikikabiliwa na tatizo ya shida ya maji.
Akizungumza na wananchi wa vijiji hivyo tarehe 17/3 , Mbunge wa Mlalo, Rashid Shangazi alimshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha ambazo zitasaidia upatikanaji wa maji katika eneo hilo.
Alisema mradi huo utakamilika mwaka huu, wananchi watapata maji safi na salama baada ya kipindi kirefu kutumia maji ya visima.
"Ndugu wananchi mradi huu utakamilika mwaka huu, tumpongeze sana Rais wetu kwa kutuletea fedha za mradi huu, hongera sana Mama Samia Mlalo huna deni," alisema Shangazi ambaye ni Katibu wa wabunge wa CCM bungeni.
Shangazi alisema kwamba anajua kwamba wananchi wa eneo hilo walikuwa wakipata shida ya maji hata pale alipowachimbia vizima virefu bado changamoto hiyo ilikuwa kubwa.
Alisema kuwa akishirikiana na marafiki wa Rashid Shangazi waliweza kuchimba visima maeneo mbalimbali ya Jimbo hilo ikiwemo Kijiji cha Mazinde kilichopo kata ya Mng'aro eneo la Magereza.
Akizungumza katika mkutano huo diwani wa kata ya Mnazi Zuberi Sechambo alimshukuru mbunge kwa kuwezesha mradi huo ambao utasaidia wananchi ambao eneo lao ni kame.
Alisema mradi huo ambao utafika kwa msereleko 'Gravity' kutoka kwenye vyanzo vya maji Mtae, utawasaidia wananchi zaidi ya 2,000 pindi utakapokamilika.







Comments
Post a Comment