📍 Yaomba barabara ya Tanga Pangani, Bagamoyo ipitie hifadhi ya Saadan
Na MASHAKA MHANDO, Pangani
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, imeishauri Wakala wa barabara nchini (TANROADS) kufanya uwezekano wa barabara ya Tanga, Pangani Makurunge wilayani Bagamoyo inapita katika hifadhi ya Taifa ya Saadan ili kuongeza watalii na kuitangaza hifadhi hiyo.
Akizungumza katika majumuisho baada ya Kamati hiyo kukagua na kutembelea mradi wa barabara ya Tanga Pangani pamoja na daraja la mto Pangani, mwenyekiti wa Kamati alisema kuichepusha barabara hiyo katika eneo jingine, hakuna tija.
Alisema Kamati ya Bunge ingependa kuona wataalamu wa Wizara ya ujenzi na Ofisi ya Makamo wa Rais Mazingira wanashirikiana kuona uwezekano wa barabara hiyo kupitia katika hifadhi ya Saadan kuliko sasa inapitia eneo jingine.
"Narudi mara ya pili, Bunge lingependa sana barabara ya kutoka Tanga ingeenda kupitia kwenye hifadhi ya Saadan itafungua mkoa kiuchumi na kuongeza idadi ya watalii," alisema na kuongeza,
"Serikali haijengi barabara kuwafurahisha wananchi, serikali inajenga barabara kufungua uchumi wa nchi, kama tunapeleka barabara halafu tunaichepusha eneo ambalo lingekuwa na tija zaidi, tunaomba mlifanyie upembuzi yakinifu mje na majibu ya msingi kwenye miradi hii ya kimkakati,".
Alisema kuwa Kamati hiyo haikatai barabara hiyo kuchepushwa katika eneo la Kwamsisi wilayani Handeni, lakini ametaka wakae na watafute namna bora itakayowezesha barabara hiyo inapitia hifadhini ili kuongeza tija zaidi kwa barabara hiyo kupitia kwenye mwambao wa bahari.
Alisema Kamati hiyo imeridhishwa na ujenzi wa daraja pamoja na ujenzi wa barabara hiyo lakini wametaka serikali kupitia Tanroads iwasimamie wakandarasi ili wamalize mapema kulingana na masharti yaliyokuwemo kwenye mkataba walioingia.
Pia mwenyekiti huyo na Kamati yake ikiwa na wajumbe wake mbalimbali wakiwemo Joyce Ndalichako, Livingston Lusinde, Mhandisi Mwanaisha Ulenge, Abubakar Assenga, wamewataka wananchi wa Pangani endapo barabara hiyo ikikamilika waitumie kuongeza uchumi wao kwa kutumia fursa za uwepo wa barabara hiyo.
Awali Mhandisi msimamizi wa barabara ya Tanga Pangani, Mhandisi Gladson Yohana alisema kuwa awali mkandarasi anayejenga barabara ya Tanga Pangani alikuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo malipo ya fedha lakini Sasa serikali tayari imemlipa na wamempa wiki mbili arejee kazini kuendelea na ujenzi wa barabara hiyo.
Alisema serikali kupitia Rais Dkt Samia Suluhu Hassan mwezi wa kumi na mbili mwaka jana ilimlipa kiasi cha shilingi bilioni 4.7 na mapema February mwaka huu amelipwa kiasi cha shilingi bilioni 10.8.
Barabara ya Tanga Pangani hadi Sasa imejengwa kwa kiwango cha lami kiasi cha kilomita 15.8 na sehemu ya kilomita 35 bado ikiwemo madaraja.




.jpg)


Comments
Post a Comment