Solar Freezer Zinavyoweza Kusaidia Kupunguza Upotevu na Kuharibika Kwa Mazao ya Chakula Baada ya Mavuno
Na Emmanuel Chibasa
Tanzania sawa na nchi nyingine zinazoendelea Duniani, inakabiliwa na upotevu mkubwa wa mazao kati ya asilimia 20 hadi 30 ya mazao ya mkulima, hupotea baada ya mavuno kutokana na wakulima kuwa na uelewa mdogo wa uhifadhi na matumizi ya teknolojia nafuu na safi kama vile nishati ya jua kwa ajili ya kuhifadhi mazao.
Upotevu wa chakula kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO), hutokea kuanzia shambani baada ya mavuno bila kujumuisha mauzo. Upotevu huo unaweza kufanywa na wakulima, katika mchakato wa uandaaji pamoja na usafirishaji kwa ajili ya uuzaji wa chakula na utupwaji, kwa upande mwingine hutokea sokoni baina ya muuzaji na mtumiaji.
Wakati hali hii ikitokea kwa wakulima hapa nchini na duniani Kwa chakula kupotea baada ya mavuno au kuharibika na kutupwa inakadiliwa kuwa kuna watu takribani Milioni 820 duniani kote wanakabiliwa na njaa.
Shirika la umoja wa mataifa la chakula na kilimo linaeleza kuwa, ni muhimu kuzuia upotevu na utupwaji wa chakula kama mkakati muhimu wa Kukabiliana na athari za mabadiriko ya tabia nchi, kwa kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi lakini pia kuongeza upatikanaji wa chakula, kuchangia uhakika wa chakula pamoja na lishe bora.
Ukosefu wa elimu ya matumizi ya nishati ya umeme jua na uwekezaji kwenye miradi ya ubunifu ya teknolojia ya nishati ya jua ambayo ni nafuu, safi na uhakika na inayohamishika kama vile matumizi ya Solar Freezer katika kuhuifadhi mazao ya wakulima wadogo baada ya mavuno, ni sababu kubwa zinayotajwa kuchangia uwepo wa tatizo la ukosefu wa usalama wa chakula na upotevu wa chakula baada ya mavuno.
Ubunifu wa solar freezer ni moja ya suluhisho inayoweza kuwasaidia na kuwawezesha wakulima wadogo na wajasiliamali katika wilaya ya Musoma na mkoa wa Mara kwa ujumla, kupunguza upotevu wa mazao ya chakula baada ya mavuno, na kukuza thamani ya mazao, hivyo kuongeza mapato kwa wakulima lakini pia kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kutokana na upoteaji wa chakula.
Licha ya ukosefu wa elimu na miradi ya nishati ya umeme jua Kwa ajili ya kuhifadhi mazao baada ya mavuno lakini wakulima hao na wawekezaji wanaweza kujifunza jinsi teknolojia hiyo inavyofanya kazi katika maeneo mengine Ikiwa ni pamoja na nchi ya Kenya ambapo Mradi wa solar freeze ulionzishwa Mwaka 2015 mpaka Leo unaendelea kuwahudumia wakulima Wadogo kama Mkakati wa kutatua upotevu wa mazao ya chakula baada ya mavuno.
MRADI WA SOLAR FREEZE KENYA
Dysmus Kisilu ni mwanzilishi na mkurugenzi mtendaji wa solar freeze mradi ambao unatoa suluhisho la upotevu wa mazao ya chakula kwa wakulima wadogo na wafanyabiashara hususani wanawake na vijana nchini Kenya
Katika taarifa za yake kupitia ripoti ya utafiti wa matumizi ya solar freeze iliyochapishwa na shirika la Equtor Initiative, Dysmus anasema mradi wa solar freeze ni ubunifu wa vyumba vya umeme jua nchini Kenya ambavyo wakulima wadogo wanatumia kuhifadhi mazao mapya kwa kupunguza joto.
Anasema ubunifu wa teknolojia hiyo ya vyumba vya baridi, unasaidia kuzuia ukuaji wa vijidudu, kupanua ukomo wa maisha ya matunda na mboga mboga kulingana na aina ya mazao kwa Kipindi cha kuanzia siku mbili (2) hadi nne (4) na imekua suluhisho kubwa kwa wakulima wa maeneo ya vijijini sehemu ambazo hazina umeme wa gridi.
Ameongeza kuwa miongoni mwa mafanikio ya mradi huo ni pamoja na kuwafikia wanawake na vijana wengi Wenye umri kuanzia miaka 18-29 ambao kwa Sasa wanamiliki na Kuendesha biashara ndogo ndogo na Kutoa mafunzo ya uendeshaji, matengenezo na utunzaji wa kiufundi wa vifaa vya umeme jua.
Pia kupunguza upotevu wa mazao mapya baada ya mavuno kwa Asilimia 90 pamoja na kuwafikia wakulima wadogo 3,000 ambao wananufaika Moja Kwa Moja huku pia ukisaidia uwezeshaji wa Kijinsia takribani Asilimia 80 au wakulima 2,400 ambao ni wanawake
HALI YA KILIMO NA UMASIKINI WA CHAKULA
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 katika ripoti ya hali ya usalama wa chakula kwa Tanzania bara, kulingana na takwimu za utafiti wa mapato na matumizi ya kaya binafsi mwaka 2017-2018 ya ofisi ya Taifa ya Takwimu Tanzania (TBS) iliyotolewa September 2024 inaonesha kuwa, Sekta ya kilimo inachangia pato la taifa kwa asilimia 26.5, asilimia 63.4 ya kaya zinajishughulisha na kilimo na asilimia 26.4 ya watu wa Tanzania bara wana umasikini wa mahitaji ya msingi, wakati asilimia 8.0 ya watu wanaishi katika umasikini wa chakula.
Shirika la chakula na kilimo la umoja wa mataifa (FAO) linakadiria kuwa, takribani theluthi moja ya chakula chochote kinachozalishwa ulimwenguni hupotea au kuharibika na athari za mazingira ni kubwa, ikiwa ni hekta bilioni 1.4 za ardhi, karibu asilimia 30 ya eneo la ardhi ya ulimwenguni linazalisha chakula ambacho hakijaliwa.
Tatizo hili linatokana na mifumo mingi ya kilimo cha chakula duniani kutokua endelevu na inaharibu ardhi ya kilimo, inachangia uzalishaji wa gesi chafuzi na upotevu wa bioanuwai na hutumia maji mengi ya ardhini.
MATUMIZI YA NISHATI KWA WAKULIMA MUSOMA
Wakati matumizi ya nishati ya jua Kupitia Mradi wa solar freeze yakionesha kuwasaidia wakulima Nchini Kenya na Kusaidia kupunguza upotevu wa mazao ya chakula baada ya mavuno lakini hali ni tofauti Kwa wakulima katika wilaya ya Musoma na Mkoa wa Mara Kwa ujumla.
Inaelezwa kuwa ukosefu wa elimu ya nishati ya umeme jua pamoja na kutokuwepo kwa miradi ya umeme jua bado wakulima wadogo na Jamii Kwa ujumla, hawana uelewa wa kutosha juu ya faida za teknolojia hii, huku changamoto nyingine ikitajwa kuwa gharama kubwa za vifaa zinapelekea watu wengi kushindwa kumudu kununua kutokana na hali ya maisha.
Butilikwa Lazaro ni afisa kilimo mkoa wa Mara, anasema ukosefu wa elimu ya matumizi ya teknolojia ya nishati ya umeme jua katika kuhifadhi mazao ya chakula kwa kutumia Solar Freezer baada ya mavuno kunachangia pakubwa kwa wakulima kuendelea kuathirika licha ya kuendelea kujishughulisha na shughuli za kilimo.
Amesema pia kukosekana kwa miradi ya teknolojia ya umeme jua katika kuhifadhi mazao baaada ya mavuno kwa kutumia Solar Freezer katika mkoa wa Mara, pia kunachangia kukwamisha wakulima na wawekezaji kukosa kujifunza jinsi teknolojia hiyo inavyofanya kazi na kama serikali inaendelea na mkakati wa kuhamasisha matumizi ya nishati jadidifu ikiwa ni pamoja na matumizi ya umeme jua katika shughuli mbalimbali za kilimo.
“ Ni kweli wakulima wadogo katika mkoa wa Mara wanakabiliwa na tatizo la upotevu wa chakula baada ya mavuno, na hii inatokana na ukosefu wa elimu juu ya matumizi ya teknolojia ya umeme jua katika kuhidhadhi chakula baada ya mavuno ili kisiharibike na tunaendelea kuhamasisha matumizi nishati mbadala kwa wakulima.
Katika mkoa wetu pia hatuna uwekezaji kwenye mradi wa umeme jua kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wadogo kuhifadhi mazao yao, nitoe rai kwa wawekezaji wasaidie kuwekeza pia katika eneo hili ili kutatua changamoto hii kwa wakulima katika mkoa wetu, ” amesema Butilikwa.
UELEWA WA WAKULIMA NA WAFANYABIASHARA
Uchunguzi wa George Marato Tv katika mahojiano na baadhi ya wakulima na wafanyabiashara umebaini kuwa, bado uelelewa wa matumizi ya nishati ya umeme jua katika kuhifadhi chakula kwa kutumia Solar Freezer uko chini, huku baadhi yao wakiwa na uelewa wa solar kwa ajili ya kupata mwanga na kuchaji simu pekee.
Sara John mkazi wa musoma na muuzaji wa mboga mboga na matunda anasema hajawahi kuiona au kusikia kuhusu Solar Freezer inavyoweza kutumika kuhifadhi mazao ili yasiharibike baada ya mavuno.
“Nimekua nikinunua mboga mboga na matunda toka kwa wakulima kwa kiwango kidogo ili kutosheleza matumizi ya muda mfupi na nimekua nikiweka mboga mboga kwenye chombo nilichoweka maji ili zisiharibike kwa haraka, ” Amesema Sara.
Peter Marwa, mkulima wa mboga mboga na matunda, anasema katika maeneo ya vijijini hajawahi kuona wakulima wanatumia solar freezer lakini amekua akiziona freezer za kawaida Zinazotumia umeme kwa wafanyabiashara wa maduka na pia kwa wanaohifadhi samaki Kwa ajili ya kusafidisha.
“Ningependa kujua hizo freezer zipo kama hizi za kawaida au zenyewe zipo tofauti? moja inaweza kuhifadhi mazao kiasi gani na kwa wakulima wangapi nikipewa elimu hiyo itanisaidia sana kupata uelewa wa matumizi yake ” Anasema Peter.
Naye Magdalena Ogutu mkazi wa Musoma ambaye ni mkulima wa nyanya pamoja na mume wake, anasema kuwa katika mtumizi ya solar anafahamu juu ya kupata mwanga, kuchaji simu pamoja na kumwagilia na freezer anazozifahamu ni zile zinazotumia umeme wa kawaida.
“Hatujapewa elimu ya hizo freezer kama wakulima katika kuhifadhi mazao yetu, nahitaji kufahamu upatikanaji wake tunapata wapi na gharama zake zikoje sababu vifaa Vya solar kidogo vina gharama” Anasema Magdalena.
Naye James Obare, mkulima wa mahindi na maharage, anasema kutokua na ufahamu wa teknolojia hiyo kunasababisha wakulima kupoteza mazao baada ya mavuno sababu hawelewi jinsi gani teknolojia hiyo inavyoweza kuwasaidia.
“Unasema inaweza kuhifadhi mazao wakati wa mavuno na baada ya mavuno, lakini hatujawahi kufundishwa wala kuona mfano wake, ingekuwa vizuri kama wangeleta hapa vijijini kwetu ili tujifunze,” anasema James.
MIKAKATI YA SERIKALI NA WADAU
Katika Kukabiliana na tatizo la upotevu wa chakula baada ya mavuno, Serikali kwa kushirikiana na shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) inatekeleza mradi wa miaka mitano wa Feed the Future Tanzania wenye thamani ya shilingi bilioni 60 (Dola za kimarekani milioni 24) kama mkakati wa kupunguza upotevu wa chakula baada ya mavuno katika mnyororo wa thamani ya kilimo cha mboga mboga na nafaka nchini Tanzania.
Mbali na Mikakati hiyo ya serikali pia shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO ) na Benki ya Dunia kwa pamoja zinapanga mipango ya sekta ya mavuno, ikiwa ni pamoja na uhifadhi kwenye baridi, kusafisha, kupanga, na kufunga hatua za uzalishaji, itatoa asilimia 47 ya dola bilioni 940 katika uwekezaji unaohitajika kumaliza njaa katika nchi za kusini mwa jangwa la sahara ifikapo 2050.
Utumiaji wa solar freezer unaweza kusaidia kufanikisha malengo kadhaa ya maendeleo endelevu (SDGs) ya ajenda ya 2030 namba 1,2,5,7 pamoja na 13.

.jpg)
.jpg)


Comments
Post a Comment