*Rufiji, Pwani.*
Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) amemtaka Mkandarasi MAC Contractor Ltd anayejenga Daraja la Mohoro lililopo Wilayani Rufiji Mkoa wa Pwani kukamilisha ujenzi wa nguzo mbili zilizobakia kwenye ujenzi wa daraja hilo kwa kuwa mvua za msimu zinakaribia.
Alisema, ujenzi wa nguzo hizo utapelekea utekelezaji wa Mradi kwa hatua inayofuata kutokukwama wakati wa Mvua.
Agizo hilo amelitoa tarehe 15.11.2024 aliporudi tena kwa mara ya pili ikiwa ni ahadi aliyoitoa wiki iliyopita alipoutembelea mradi huo.
Mhandisi Seff, amemtaka Mhandisi Mshauri wa TREECO Mhandisi Emmanuel Mahimbo kumsimamia Mkandarasi MAC ili amalize kazi kwa Wakati.
Mhandisi Mahimbo alieleza kuwa tatizo kubwa la Mkandarasi ni kutokua na malighafi za Ujenzi kama Cement hivyo kupelekea baadhi ya kazi kusuasua.
Vile vile Mhandisi Seff alitembelea kwa mara ya pili Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Utete-Kingupira (32km) inayojengwa kwa Kiwango cha Changarawe kwa kutumia Teknolojia Mbadala ya ECOROADS na Mkandarasi NRST LIMITED CIVIL WORKS CONTRACTOR JV DASHAS COMPANY LIMITED
Mhandisi Seff hakuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa Mradi huo na kumuelekeza Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Rufiji Mhandisi Nicolaus Ludigery kuhakikisha Mkandarasi NRST awasilishe programu ya kazi inayoonesha namna atakavyofidia siku zilizopotea na kukamilisha kazi kwa wakati, vinginevyo hatua za kimkataba zitachukuliwa.
Mradi wa ujenzi wa barabara ya Utete-Kingupira umepangwa kukamilika mwezi Aprili 2025.




