Serikali ya awamu ya 6 inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan imepongezwa kwa kuanzisha sheria mpya wa manunuzi ya umma na kuboresha mfumo wa utangazaji zabuni ambao utaleta tija kubwa kwa jamii.
Pongezi hizo zimetolewa jana na Mkuu wa Wilaya ya Uyui, Mohamed Mussa Mtulyakwaku kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo Paul Chacha alipokuwa akifungua semina ya siku 1 ya mafunzo ya sheria mpya ya manunuzi ya umma kwa madiwani na watumishi wa halmashauri ya Wilaya hiyo.
Amesema kuwa mfumo huo umeboresha kwa kiasi kikubwa suala zima la utangazaji zabuni za miradi ya umma na kudhibiti mianya ya rushwa katika utoaji zabuni hizo kwa wakandarasi.
Aidha amepongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa kuleta mafunzo hayo kwa Madiwani na Wataalamu wa halmashauri hiyo ili kuhakikisha wanafanya maamuzi sahihi ya manunuzi kwenye miradi ya wananchi.
DC amesisitiza kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kwa kuwa sheria mpya ya manunuzi ya umma inataka uwazi katika kila hatua, jambo ambalo linapaswa kusimamiwa kwa dhati na kutoingiza ujanja ujanja wa namna yoyote ile.
‘Tunampongeza sana Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha sheria ya manunuzi ya umma na kuanzisha mfumo mpya wa manunuzi ambao utanufaisha wananchi kupitia shughuli zao za kiuchumi’, ameeleza.
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Said Ntahondi ameeleza kufurahishwa na mfumo huo mpya wa manunuzi ya umma (NeST) kwa kuwa utaharakisha utekelezaji miradi ya maendeleo katika halmashauri hiyo na kudhibiti matumizi mabaya.
Aidha amebainisha kuwa mfumo huo umezingatia ibara ya 111 ya ilani ya uchaguzi kwenye suala la maadili ya viongozi kwa kuwa unasisitiza suala la uadilifu kwa viongozi na watumishi katika utoaji zabuni za miradi ya umma.
Akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Meneja wa Mamlaka hiyo Kanda ya Magharibi na Kati Mhandisi Summa Atupele amesema kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kwa kuwa yatawajengea uelewa mpana wa mfumo huo.
Amebainisha kuwa mfumo huo unaenda sambamba na utekelezaji ilani ya uchaguzi ya chama ibara ya 231 kwa kuhakikisha mahali popote zabuni itakapotekelezwa wakazi wa eneo hilo wananufaika ipasavyo na si vinginevyo.
Aidha mfumo huo umetoa kipaumbele kwa wazabuni wazawa kunufaika na miradi yote itakayotekelezwa hapa nchini na rasilimali au mahitaji yote ya zabuni hizo yatoke katika maeneo husika.
Mhandisi Summa amesisitiza kuwa sheria hii ya mfumo mpya wa NeST ni fursa muhimu sana kwa wakandarasi na jamii kwa ujumla hivyo akashauri madiwani na watumishi wa halmashauri hiyo kuitumia ipasavyo.




