Bashe ameyaeleza hayo katika mwendelezo wa ziara yake ya kikazi Mkoani Tabora ambapo ametembelea eneo la mradi wa Umwagiliaji wa Mwasimbo Igunga, Mwampuli, Mwanzugi na Makomero.
Waziri Bashe, ameeleza kushangazwa na hatua ya baadhi ya wananchi wa halmashauri yaNzega vijijini kupinga utekelezaji wa miradi ya skimu za umwagiliaji unaohusisha ujenzi wa miundombinu ya bwawa la Nsembo, ujenzi wa barabara, madaraja madogo na mitaro ya kupitisha maji pembezoni mwa barabara.
Wananchi wa eneo hilo wanapinga miradi hiyo kwa imani potofu kuwa inapingana na mila na sehemu inapopita miradi hiyo ni maeneo ya matambiko hivyo iondolewe.
“Hii inashangaza sana ndugu zangu wa Nzega vijijini ipo haja serikali kuongeza utoaji elimu, haiwezekani wananchi wanasimama na kudai hawataki barabara, hawataki miundombinu, wanachotaka ni ngoma za asili na matambiko, hivyo hatua zinazochukuliwa na serikali ni kuharibu mila,”ameeleza kwa Masikitiko waziri Bashe
Akiwa wilayani Igunga Waziri Bashe, ameahidi kutuma timu ya wataalamu kufanya utafiti katika ujenzi wa bwawa la kukusanya maji kutokana na uwepo wa maji mengi wakati wa mvua katika maeneo hay sanjari na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa wataalam wa Wizara hiyo watakapofika kufanya utafiti.
"Ninawaomba ndugu zangu wataalam watakapofika muwape ushirikiano,bwawa litakapojengwa mtawekewa maeneo ya kunyweshea mifugo lengo ni kuhakikisha mifugo haingii mashambani" alisema Waziri Bashe
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Umwagiliaji Raymond Mndolwa,amesema Tume ipo katika hatua za mwisho kuanza utekelezaji wa mradi wa skimu ya Mwamapuli iliyopo katika Kijiji cha Mwanzugi, kata ya Igunga wilaya ya Igunga Mkoa wa Tabora.
Skimu hiyo ilijengwa kwa mara ya kwanza mwaka 1968 hadi mwaka 1970 lakini bwawa lilikamilika mnamo mwaka 1986 hadi mwaka 1994, mifereji na miundombinu ya shambani ilijengwa na jumla ya hekta 630 zilianza kumwagiliwa Katika mwaka wa fedha 2024/2025.
“Serikali kupitia Tume imedhamiria kuboresha na kuendeleza skimu ya Mwampuli ambapo jumla ya hekta 1,557 zitajengewa miundombinu ya umwagiliaji na kufanya skimu kuwa na jumla ya hekta 2,187,”amesema Mndolwa
Kwa Mujibu wa Mndolwa,Zabuni ya mradi huo tayari umeshatangazwa kwa ajili ya kumpata Mkandarasi atakaye fanya shughuli ya ujenzi.
Kwa upande wa mkazi wa eneo hilo, Jilala Shomba, amesema kuwa wapo tayari kwa miradi inayoletwa na serikali katika maeneo yao.











