Na Shomari Binda-Musoma
MWENYEKITi wa Machifu mkoa wa Mara Chifu Deus Masanja ametoa ushauri kwa Chama cha Mapinduzi ( CCM ) kujiepusha na Rushwa wakati wa uchaguzi wa ndani wa chama hicho.
Kauli hiyo ameitoa leo mbele ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa chama hicho Taifa Fadhil Maganya leo septemba 11 alipopita kuwasalimia machifu hao walipokuwa wakifanya kikao ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mara.
Amesema Rushwa inapelekea kupata viongozi wasiofaa na ambao hawatakuwa na moyo wa kuweza kuwatumikia wananchi.
Chifu Masanja amesema eneo ambalo wanapaswa kuliangalia ni kuhakikisha wanawake hawakatwi majina yao wanapojitokeza kugombea.
Amesema wanawake wameonyesha kusimamia vizuri masuala ya uongozi kama anavyofanya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan hivyo wanastahili kupewa nafasi.
Kiongozi huyo wa machifu mkoa wa Mara amesema Rushwa isiwe kikwazo kwa wanawake kupata nafasi za uongozi pale wanapojitokeza kuomba nafasi.
" Nashukuru Mwenyekiti wa Wazazi kuja kutusalimia na kwa niaba ya machifu wa mkoa wa Mara tunaomba utupelekee salam zetu kwa Rais Dkt.Samia.
Jambo la muhimu ni kupambana na vitendo vya Rushwa na kuepuka kuwakata majina wanawake watakaojitokeza kugombea"Amesema.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Fadhil Maganya amesema amefurahi kukutana na machifu hao na atafikisha salam zao kwa Rais Samia na ushauri walioutoa.
Mwenyekiti huyo wa jumuiya ya wazazi yupo kwenye ziara ya kikazi ya siku 2 mkoani Mara akiambatana na viongozi wa chama na jumuiya za CCM mkoa.


