Jinsi Grumeti Fund Inavyowawezesha Wananchi Ujuzi na Rasilimali Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabia Nchi Serengeti na Bunda.
Na Emmanuel Chibasa
Athari za mabadiliko ya tabia nchini zimeendelea kuathiri
shughuli nyingi za kiuchumi hususani kilimo na ufugaji hapa nchini na duniani kwa ujumla na athari hizi pia zimekua zikiwakumba wakazi wa wilaya ya Serengeti mkoani
Mara ambao pia ni jamii ya wakulima na wafugaji.
Miongoni mwa changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi inayowakumba
wananchi katika eneo hilo ni kupungua kwa malisho ya wanyama kutokana na
kubadirika kwa misimu ya joto na mvua na hivyo jamii hiyo kuathirika pakubwa
kutokana na kutegemea shughuli za kilimo na ufugaji kujikimu kimaisha.
Changamoto hizi kwa sasa zimeanza kupatiwa ufumbuzi baada ya
shirika lisilo la kiserikali la Grumeti Fund linalofanya kazi za kuhifadhi Pori
tengefu la Grumeti lililopo magharibi mwa hifadhi ya Taifa ya Serengeti
kuanzisha mradi mpya unaojulikana kama “Climate-resilience and Livelihood
Improvement Program” (CLIP) kama mkakati wa kuiwezesha jamii hiyo kukabiliana
na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa katika jarida la Sauti
ya Grumeti, Chapisho la 14 taarifa za mwezi Januari hadi Machi 2024 ambalo pia
ni jarida la Uhifadhi na Maendeleo ya Jamii, inaeleza kuwa mradi huo
umeanzishwa kupitia idara yake ya maendeleo ya jamii ili kuwawezesha wafugaji
wa vijiji vya pembezoni na Mapori ya akiba na Ikorongo-Grumeti, kwa kuwapatia
ujuzi na rasilimali zinazohitajika kujihusisha na ufugaji wa Ng’ombe wa maziwa
huku wakihifadhi Mazingira.
Mbali na lengo hilo pia taarifa hiyo inaeleza kuwa, mradi
huo umejikita kukuza matumizi ya mbinu za kilimo-hai na kuhimiza uzalishaji wa
bidhaa za maziwa zenye thamani kubwa kama vile Mtindi,Jibini na bidhaa nyingine
za Maziwa ili kuimarisha uchumi wa wananchi.
Katika kutekeleza mradi huo, Maafisa wa Program ya Ustawi wa
biashara vijijini ya Grumeti Fund, Nelson Petro pamoja na Philip Simel, wamekua
wakifanya kazi kwa ukaribu na wataalam wa mifugo ngazi ya Wilaya katika utoaji
wa elimu ya ufugaji, Utengenezaji wa mabanda ya Kisasa na upatikanaji wa
malisho kwa ajili ya Ng’ombe hao.
Mzee Kitana ni mkazi wa kijiji cha Mugeta ambaye ni miongonimwa
wanufaika wa mradi huo, anasema kuwa kwa miaka mingi alikua anafuga ng’ombe
wengi bila tija lakini baadae aliamua kuanza kufuga ng’ombe wa maziwa kutokana
na wepesi wa kuwahudumia na uangalizi na alipoona fursa kutoka Grumeti Fund
hakusita kufanya maombi na anashukuru kupata fursa hiyo ambayo inaendelea
kuboresha maisha ya familia yake.
Tarehe 14 mwezi wa Pili 2024 wajasiliamali hao walipokea
ng’ombe wa maziwa chini ya mradi huo na uzinduzi rasmi wa mradi huo ulifanyika
7/03/2024 katika kijiji cha Mugeta na Nyichoka wilaya ya Bunda na Serengeti.
Mwaka 2023 Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kilizindua
ripoti ya Mabadiliko ya tabia nchi 18/5/2023 ripoti iliyozinduliwa na
Mkurugenzi wa kituo hicho Anna Henga.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti, Mkurugenzi huyo
alisema kwa mujibu wa utafiti walioufanya unaonesha kuwa wanawake na watoto
wameathirika zaidi kutokana na mabadiliko hayo, kutokana na mtindo wa kuhama au
unaofanywa na familia ili kupata mahitaji ya chakula, Mazingira,Maji safi na
salama, Afya pamoja na Elimu jambo ambalo pia linasababisha badhi ya watoto
kutopata haki ya elimu huku baadhi ya wazazi wakitelekeza familia kutokana na
hamahama hiyo.
Wanyamapori wanatoa mchango kwenye sekta ya utalii ambayo
inaingiza mapato kwa taifa na ongezeko la watu, mahitaji makubwa ya ardhi na
mabadiriko ya tabia nchi na magonjwa ya mifugo vimechangia kuleta mabadiriko
pia katika maeneo ya wafugaji.
Wafugaji ambao miaka iliyopita walikua wakihamahama sasa
wataendelea kuishi sehemu za kudumu na kujihusisha pia na shuguli za kilimo na
ufugaji kupitia mradi huo.
Chanzo: Grumeti Fund na Lhrc.

Comments
Post a Comment