KATAMBI ATOA WITO KWA JAMII KULINDA MAADILI, ASEMA SHERIA ZITACHUKUA HATUA DHIDI YA UHALIFU WA KIMAADILI
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi ametoa wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika kulinda maadili, uzalendo na utamaduni wa taifa, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya makosa yanayohusiana na mmomonyoko wa maadili katika jamii.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jun 23,2026 Jijini Dodoma kuhusu ongezeko la matukio yanayohusiana na maadili mitandaoni na katika jamii, Katambi amesema kuwa Sheria ya Kanuni ya Adhabu ina vifungu vinavyohusiana na makosa dhidi ya maadili ya jamii na kwamba Serikali inaendelea kuzitekeleza kikamilifu.
Amesema baadhi ya makosa hayo ni pamoja na vitendo vya kuingilia maumbile kinyume cha sheria, ubakaji, ulawiti, ukahaba pamoja na makosa mengine ya ukatili wa kijinsia na uvunjifu wa amani, akibainisha kuwa vyote vinaainishwa kisheria na vinachukuliwa hatua.
Katambi amesisitiza kuwa ongezeko la maudhui yasiyofaa katika mitandao ya kijamii ni changamoto inayohitaji ushirikiano wa jamii, wazazi, taasisi za elimu, viongozi wa dini na vyombo vya habari ili kuzuia mmomonyoko wa maadili, hasa kwa watoto na vijana.
Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kiuchumi kupitia mikopo kwa wanawake na vijana ili kupunguza vishawishi vya kujihusisha na vitendo visivyo halali, huku akisisitiza kuwa ajira na fursa mbadala zipo kwa wananchi.
Aidha, ameeleza kuwa hatua za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi ya wote wanaojihusisha na vitendo vinavyokiuka sheria, akisisitiza kuwa jamii yote inapaswa kuwajibika katika kulinda maadili ya Kitanzania na mustakabali wa taifa.
Kwa upande wake waziri wa maendeleo ya jamii jinsia wanawake na Makundi Maalumu, Dkt. Dorothy Gwajima Amesema kumekuwa na changamoto ya kile kinachoitwa mmomonyoko wa maadili, ambao unajumuisha tabia na mienendo inayokiuka mila, desturi na maadili ya jamii.
Amesisitiza kuwa baadhi ya vitendo vinavyoleta mjadala mkubwa katika jamii ni pamoja na uhalifu wa kijinsia, ubakaji na ulawiti hasa kwa watoto, ambavyo vimepewa uzito mkubwa kisheria na kijamii.
Aidha,ameeleza kuwa malezi ya watoto yanapaswa kuanzia nyumbani, ambapo wazazi na walezi wana jukumu la kuwalea watoto katika maadili mema, heshima na utii kwa sheria za nchi na maadili ya kijamii.
Amesema kuwa malezi si tu kuwapatia watoto mahitaji ya msingi, bali pia kuwajenga kimaadili, kiimani na kimaisha ili wawe raia wema wa baadaye.
Serikali inaihimiza Jamii kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa za matukio ya uhalifu kupitia njia rasmi, ikiwemo vituo vya polisi na mifumo ya kuripoti mtandaoni, ili hatua stahiki zichukuliwe kwa mujibu wa sheria.



Comments
Post a Comment