Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na Ofisi ya DPP tarehe 23 Juni 2026, faili la uchunguzi wa awali lililowasilishwa na Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) limefanyiwa tathmini ya kina na kubaini kuwepo kwa ushahidi wa kutosha wa kuendelea na hatua za kisheria dhidi ya watuhumiwa.
DPP amesema kuwa wanafunzi wanaohusishwa na tukio hilo watakabiliwa na mashtaka 16 ya mauaji, yakitokana na vifo vya wanafunzi 16 vilivyoripotiwa kufuatia ajali hiyo ya moto iliyotikisa taifa la Kenya.
Katika taarifa hiyo, DPP ameonesha wasiwasi mkubwa kuhusu ongezeko la matukio ya uchomaji moto na vitendo vingine vya uhalifu vinavyoripotiwa katika taasisi za elimu nchini humo. Aidha, amesisitiza kuwa watu wote watakaobainika kuhusika na makosa ya aina hiyo watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria.
Ofisi hiyo pia imetoa salamu za rambirambi kwa familia za marehemu, marafiki pamoja na jamii ya shule ya Utumishi Girls Academy iliyoathiriwa na tukio hilo. DPP ameahidi kuendelea kusimamia mchakato wa haki kwa njia ya uchunguzi na ushahidi wa kitaalamu.Taarifa hiyo imehitimisha kwa kusisitiza dhamira ya Ofisi ya DPP katika kulinda utawala wa sheria, maslahi ya umma na kuhakikisha uwajibikaji kwa wote watakaothibitika kufanya vitendo vya uhalifu.
Tukio la moto wa Utumishi Girls Academy limeendelea kuvuta hisia za wananchi wengi nchini Kenya kutokana na ukubwa wa madhara yake na idadi ya maisha yaliyopotea. Serikali na vyombo vya sheria sasa vinatazamiwa kuhakikisha haki inapatikana kwa waathirika na familia zao.



Comments
Post a Comment