NA MASHAKA MHANDO, Tanga
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Tanga, imefichua kukwama kwa miaka miwili kwa mradi wa madarasa na vyoo katika Shule ya Sekondari Chongoleani Jijini Tanga.
Mradi huo wa thamani ya Sh. 93,816,506, ulishindwa kuanza utekelezaji tangu fedha zilipotolewa Machi 4, 2024 kutokana na kasoro kubwa za kiutawala na mfumo wa manunuzi wa halmashauri ya Jiji la Tanga.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Tanga, Ramadhani Ndwata, aliwaambia waandishi wa Habari ofisini kwake Leo Juni 8 2026 wakati wa kutoa taarifa ya utendaji wa robo ya kwanza ya mwaka (Januari–Machi, 2026), ambapo alisema uingiliaji kati wa taasisi hiyo umeokoa hasara ya jumla ya Sh. 116,216,506 katika sekta ya elimu.
Uchunguzi wa TAKUKURU ulibaini kuwa, makadirio ya bei ya vifaa vya ujenzi wa madarasa hayo mawili yalikuwa chini ya bei halisi ya soko, hali iliyosababisha mfumo wa manunuzi wa kielektroniki wa Serikali (*NeST*) kukataa zabuni zote na kukwamisha maendeleo ya wanafunzi wa shule hiyo.
"Kwa upande wa ujenzi wa vyoo vya Sh. milioni 40 Chongoleani, hakukuwa na maandalizi kabisa ya makadirio ya gharama (quotation) na taratibu hazikuanzishwa. Tulichukua hatua za dharura kuimarisha uwajibikaji na kwa sasa mradi umerudi na upo katika hali nzuri," alisema Kamanda Ndwata.
Katika eneo lingine, TAKUKURU imeingilia kati mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari Kwabastola wilayani Muheza wenye thamani ya Sh. 1,063,280,028 ambapo ilibainika kuwepo kwa changamoto za kiufundi.
Kamanda Ndwata alieleza kuwa, taasisi hiyo ililazimisha marekebisho ya milango kupakwa vanish, kurekebisha mikanda ya gypsum, pamoja na kufuatilia vitanda 80 vilivyokuwa vimenunuliwa lakini vikahamishwa "kimyakimya" kwenda Shule ya jirani ya Muheza High School kwa kisingizio cha mradi kutokamilika ambapo sasa vimerudishwa shuleni hapo.
Kwa ujumla, katika kipindi cha miezi mitatu, TAKUKURU Tanga imefanya ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za umma katika miradi 49 ya maendeleo kwenye sekta za Maji, Afya, Elimu, Barabara na Utawala yenye thamani ya Sh. 506,730,035,914.33.
Kuhusu upande wa mashtaka na uchunguzi kitalamu, ofisi ya mkuu wa mkoa wa taasisi hiyo ilipokea jumla ya malalamiko 133, ambapo malalamiko 100 sawa na asilimia 75.2 yalihusu vitendo ghafi vya rushwa, na majalada ya uchunguzi yameshafunguliwa kwa hatua za dharura.
Ndwata alihitimisha kwa kusema kuwa mashauri 11 mapya yamefunguliwa mahakamani, huku mashauri mengine 18 yakiendelea kurindima kwenye korido za sheria mkoani Tanga, huku akitoa wito kwa wananchi kupitia klabu 163 za wapinga rushwa kuacha kujihusisha na makosa hayo.


Comments
Post a Comment