Na Mwandishi Wetu, Mkinga
MBUNGE wa Jimbo la Mkinga, mkoani Tanga, Twaha Mwakioja ameingilia kati tatizo la vijana wengi wanaoishi maeneo ya mpakani wilayani humo kukabiliwa na changamoto ya kukosa mikopo kutokana na kucheleweshewa namba za NIDA.
Hali hiyo ilibainishwa na Mjumbe wa Bodaboda, Ali Selemani Rasi, wakati wa kikao maalum kati ya Mbunge wa Jimbo la Mkinga, Mhe. Twaha Mwakioja, na waendesha pikipiki wa kijiwe cha Duga Maforoni kilichofanyika leo Juni 7, 2026.
Rasi alisema vijana wa Duga Maforoni wanakosa fursa za kupata mikopo inayotolewa na Serikali ya asilimia 10 kutoka kwenye mapato ya ndani ya halmashauri kwa kuwa hawana vitambulisho hivyo vya taifa.
"Mheshimiwa Mbunge, sisi vijana tunaoishi mipakani tuna tatizo kubwa la kukosa namba za NIDA ambazo zinatufanya tushindwe kupata mikopo ya vijana," alisema Rasi na kumuomba Mbunge awasaidie ili waweze kupata mikopo hiyo kama wenzao wengine nchini.
Akijibu malalamiko hayo, Mbunge Mwakioja alitoa agizo la kimkakati akisema kuwa kuanzia kesho taratibu zote zitakwenda kwa kasi ili kuwasaidia vijana hao wapate haki yao ya msingi. Alisema haiwezekani Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa mikopo kwa ajili ya kuwawezesha vijana, wanawake na makundi maalum huku vijana katika jimbo lake wakikwama.
"Jambo hili tunataka liende haraka sana. Ndani ya wiki mbili zijazo, nataka kila kijana awe amepata namba yake ya NIDA. Haiwezekani vijana wetu wakwame na wakose fursa za mikopo ya kiuchumi mtaani kwa sababu tu ya urasimu wa kukosa vitambulisho," alisisitiza Mbunge Mwakioja.
Malalamiko ya kukosa namba za NIDA kwa wananchi wa Wilaya ya Mkinga, hasa kata za Moa, Duga Sigaya, Mwakijembe na Duga Maforoni zilizopo mpakani mwa Kenya na Tanzania, yamekuwa mengi na utatuzi wake umekuwa ukienda taratibu kutokana na usalama wa mwingiliano mkubwa wa jamii zinazoishi katika maeneo hayo ya mipakani.
Katika kikao hicho kilichohudhuriwa pia na Diwani wa Kata ya Duga, Mhe. Jumaa Abdallah Rioba, Mbunge Mwakioja alikabidhi mabati ya jumla ya Sh. 600,000 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa banda la abiria, mradi uliopata kibali cha dharura kutoka TANROADS.
Mhe. Mwakioja alikubali ombi la risala ya vijana iliyosomwa na Haji Selemani, na kuahidi kuwanunulia TV ya kisasa, king'amuzi, pamoja na jokofu (friji) la kuuzia vinywaji ili kuwaongezea kipato, huku akiahidi kushirikiana na Diwani kutoa mafunzo ya usalama barabarani na leseni kama walivyoomba.
Hata hivyo, Mbunge aliweka sharti akitaka kituo hicho cha bodaboda Duga Maforoni kutumika kama kituo cha Amani na hifadhi ya mazingira, ambapo madereva hao watakuwa mabalozi wa kudhibiti utakatishaji na upitishaji wa dawa za kulevya kama mirungi, bangi na kokeini mpakani.
Suala lingine lililoibuka kwenye kikao hicho liliwasilishwa na kijana Mwanakombo Twaha Mbwana, aliyehoji hatma ya vijana 32 waliopata mafunzo ya Uaskari Misitu mkoani Mwanza lakini hadi sasa wapo mtaani hawajui hatma yao baada ya mafunzo hayo.
Mbunge Mwakioja aliahidi kuwasiliana moja kwa moja na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, ili kuona vijana hao wanawekwa kwenye daraja gani la ajira, huku akiwataka wananchi kuendelea kumuunga mkono Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Naye mwendesha bodaboda, Suna Mwasega, alimshukuru Mbunge kwa usimamizi wage thabiti na kuwa karibu na wananchi tofauti na mtangulizi wake, huku kikao hicho kikifungwa kwa hamasa kubwa na Duga Maforoni ikitakiwa kujiandaa na mkesha wa Mwenge wa Uhuru 2026 mara baada ya kumaliza kukimbizwa wilayani humo.
Katika hatua nyingine mbunge Mwakioja alisema serikali imetoa kiasi cha Shilingi milioni 980 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na shule mpya ya sekondari katika mji wa Horohoro.
Mhe. Mwakioja alifafanua mbele ya umati wa wananchi kuwa, kati ya fedha hizo, jumla ya Sh. milioni 680 zitaenda moja kwa moja kwenye ujenzi wa kituo cha afya cha kisasa, huku Sh. milioni 300 zikitumika kujenga Shule ya Sekondari ya Horohoro Kijijini.
Hatua hiyo inatajwa na wadau wa maendeleo wilayani Mkinga kuwa ni ukombozi mkubwa kwa akina mama na watoto waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za kitabibu na elimu nchi jirani ya Kenya.
Kuhusu changamoto sugu ya upatikanaji wa maji safi na salama wilayani humo, Mbunge Mwakioja alishusha data za kiufundi kuhusu mradi mkubwa wa maji wa kimkakati kutoka Tanga hadi Horohoro wenye thamani ya Sh. bilioni 35.
Alieleza kuwa mradi huo kwa sasa umefikia hatua nzuri ambapo mafundi wapo site wakiendelea na kazi ya utandikaji wa mabomba makuu ili kusogeza huduma hiyo kwenye makazi ya watu.
"Ndugu zangu, hakika suala la maji tayari tumelipatia ufumbuzi wa dhati kitalamu. Hizi bilioni 35 zitafikisha maji ya uhakika hadi huku Horohoro mpakani, na kero hii ya muda mrefu inakwenda kubaki kuwa historia tu mtaani kwetu," alisema Mbunge Mwakioja huku akishangiliwa.
Uchunguzi wa MaratoTV unaonyesha kuwa ujio wa miundombinu hiyo mipya ya afya, elimu, na maji mpakani utachochea kwa kasi ukuaji wa uchumi wa wilaya ya Mkinga na kuongeza usalama wa jamii kutokana na upatikanaji wa huduma za kijamii za kiwango cha juu.





Comments
Post a Comment