Wanaitende Mtaoga Maji Mpaka Mtachubuka-Mwalunenge

GEORGE MARATO TV
0


MBUNGE wa Jimbo la Mbeya Mjini, Patrick Mwalunenge, amezindua rasmi mradi wa uchimbaji wa visima vya maji katika Kata ya Itende, Wilaya ya Mbeya, mkoani Mbeya, ikiwa ni hatua ya kupunguza changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa eneo hilo ambapo amesema wataoga maji mpaka wachubuke.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mwalunenge amesisitiza dhamira yake ya kuleta mabadiliko ndani ya kipindi chake cha uongozi, akibainisha kuwa hatarajii kuacha ahadi yoyote bila utekelezaji.


“Nataka miaka yangu mitano Itende ibadilike. Mkataba mlionipa ni wa miaka mitano, na mambo yote niliyoahidi lazima niyatekeleze ndani ya kipindi hicho,” amesema Mwalunenge.

Ameeleza kuwa kila kisima kitagharimu takribani shilingi milioni 12 hadi kukamilika kwake ambapo amewataka wananchi kushiriki katika utunzaji wa miundombinu hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kuwahudumia ipasavyo.

“Tukitunze hiki kisima ili hata tukipata fedha nyingine tuweze kuongeza visima vingine zaidi,” ameongeza.




Mbunge huyo amesema kuwa fedha za mradi huo zinatokana na Mfuko wa Jimbo, akisisitiza kuwa utekelezaji huo ni sehemu ya kuwajibika kwa wananchi waliomchagua.

Aidha, amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuhamasisha na kusukuma mbele miradi ya maendeleo nchini.

“Mtu wa kwanza kumshukuru ni Rais Samia Suluhu Hassan, kwa sababu anataka tukatatue shida za wananchi. Serikali yake inaendelea kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu ikiwemo maji,” amesema.

Amebainisha pia kuna mradi mkubwa wa maji wa Kiwila ambao upo Kwenye mchakato na  unaotarajiwa kusambaza huduma hiyo katika vijiji vyote vya Mbeya, ambao ukikamilika utakuwa suluhisho la kudumu kwa changamoto ya maji.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Itende Kati, Metson Shongwe, amemshukuru mbunge huyo kwa kuwafikia wananchi na kuanzisha mradi huo muhimu.

Naye Chifu wa eneo hilo, Juma Jojo, amesema ongezeko la idadi ya watu limekuwa likichangia upungufu wa huduma ya maji safi na salama, hivyo kisima hicho kitasaidia kupunguza tatizo hilo kwa kiasi kikubwa.

Diwani wa Kata ya Itende, Andambike Mwakyusa, amesema changamoto ya maji ilikuwa miongoni mwa vipaumbele vilivyowasilishwa kwa mbunge huyo wakati wa kampeni, akibainisha kuwa utekelezaji wa mradi huo ndani ya kipindi kifupi unaonesha dhamira ya kweli ya kutatua kero za wananchi.

Huduma ya maji imeendelea kutajwa kuwa mhimili muhimu katika maisha ya mwanadamu, ikizingatiwa kuwa maji ni uhai na yanachukua nafasi kubwa katika shughuli zote za kila siku za binadamu, kuanzia matumizi ya nyumbani hadi uzalishaji.




Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top