KAMPUNI ya kimataifa ya usafirishaji wa mizigo ya Silent Ocean, maarufu kama “Simba wa Bahari”, imetangaza kuendelea kuwa mdhamini mkuu wa Bunge Marathon kwa kipindi cha miaka mitano zaidi, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi na kulinda afya zao.
Akizungumza leo Aprili 18, 2026 katika Viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma wakati wa mbio hizo, Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Ndg. Mohammed Soloka, amesema Kampuni hiyo imejipanga kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu na Serikali pamoja na jamii katika nyanja mbalimbali za maendeleo.
“Tutaendelea kuwa sehemu ya Serikali yetu kwa kushirikiana katika kuimarisha huduma kwa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata elimu na huduma bora kupitia kampuni ya Silent Ocean,” amesema Soloka.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, ameipongeza kampuni hiyo kwa mchango wake mkubwa uliowezesha mafanikio ya Bunge Marathon msimu wa tatu, akieleza kuwa udhamini huo umekuwa nguzo muhimu ya mafanikio ya tukio hilo.
“Kwa namna ya kipekee, kampuni ya Silent Ocean imekuwa mhimili mkuu wa mafanikio ya Bunge Marathon. Bila wao, huenda tukio hili lisingefanyika kwa ubora, urahisi na ufanisi ulioshuhudiwa,” amesema Mwinjuma.
Naye Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu, ameishukuru kampuni hiyo kwa mchango wake mkubwa, akisema umechangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha tukio hilo kwa mafanikio na furaha ya pamoja.
“Ushirikiano kati ya Bunge na wadhamini mbalimbali umeleta matokeo chanya ambayo taifa linajivunia. Mchango wao umeonesha mshikamano na uzalendo katika kuunga mkono maendeleo ya nchi,” amesema Spika Zungu.
Mgeni Rasmi wa mbio hizo, Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, amesisitiza umuhimu wa amani na mshikamano, akibainisha kuwa Bunge Marathon ni jukwaa muhimu la kuunganisha taasisi mbalimbali na kuhamasisha afya bora kwa wananchi.
“Bunge Marathon inaunganisha taasisi mbalimbali na kujenga taifa lenye afya bora na mshikamano. Afya ya wananchi ni msingi wa uzalishaji na maendeleo endelevu,” amesema.
Aidha, ameongeza Aidha, amewashukuru viongozi wakuu wa nchi kwa kuendelea kudumisha amani na umoja, akisema:
“Namshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa uongozi wao imara na maono makubwa katika kudumisha amani nchini Tanzania.”. amesema
Bunge Marathon msimu wa tatu imefanyika leo katika Viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma, ikihusisha viongozi, wabunge na wananchi mbalimbali walioshiriki katika mbio za kilomita 5, 10 na 21.










