RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameielekeza Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kuhakikisha kuwa miundombinu ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano inakamilika kufika katika wilaya zote nchini ifikapo mwezi Desemba mwaka huu kama ilivyopangwa.
Rais Samia ametoa maelekezo hayo leo jijini Dodoma wakati akizindua minara 758 ya mawasiliano pamoja na maunganisho ya mkongo katika wilaya 85, hatua iliyowezesha pia kukabidhi rasmi Mkongo wa Mawasiliano Serikalini.
Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha huduma za mawasiliano zinafika hadi ngazi ya kata na vitongoji, ili kila Mtanzania, bila kujali alipo, anufaike na fursa za uchumi wa kidijitali.
“Teknolojia ya habari na mawasiliano ni sekta ya kimkakati inayochochea ajira, kuongeza tija katika uzalishaji na kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika miundombinu ya mawasiliano,” amesema Rais Samia.
Ameongeza kuwa Mkongo wa Taifa umeunganisha mikoa yote ya Tanzania Bara na wilaya nyingi, hatua inayolenga kuimarisha huduma za kidijitali nchini.
Aidha, Rais Samia ameielekeza Wizara ya Mawasiliano kuhakikisha huduma hizo zinazingatia maadili, mila na tamaduni za Kitanzania ili matumizi ya teknolojia yawe na manufaa kwa jamii bila kupoteza misingi ya utu na uzalendo.
Pia amesisitiza umuhimu wa vijana kunufaika na uwekezaji huo kwa kukuza ubunifu, ujuzi wa kidijitali na kuongeza fursa za ajira.
“Dunia ya teknolojia ni yao vijana. Ni lazima tuwawezeshe ili waweze kukua kiuchumi na kijamii,” amesema.
Rais Samia pia ametangaza kuwa Serikali itatenga fedha kusaidia kampuni changa za vijana ili ziweze kupata mitaji na kuchangia maendeleo ya uchumi wa kidijitali.
Akitoa taarifa ya utekelezaji, Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), Mhandisi Peter Mwasalyanda, amesema mradi wa ujenzi wa minara 758 ulianza Mei 13, 2023.
Amesema mradi huo umetumia Shilingi bilioni 126, ambapo bilioni 55 ni mkopo kutoka Benki ya Dunia kupitia Mradi wa Tanzania ya Kidijitali, na bilioni 71 ni fedha za ndani kupitia UCSAF.
Kwa mujibu wake, minara hiyo imejengwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na kampuni za mawasiliano ambapo Yas imejenga minara 261, Vodacom 190, Airtel 169, TTCL 104 na Halotel 34.
Aidha, amesema pia mradi wa kuboresha minara 304 kutoka 2G kwenda 3G na 4G ulikamilika Machi 2025.
Kwa upande wake, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema Serikali inaendelea na ujenzi wa minara 201 katika kata 201 zenye vijiji 263, mradi unaotarajiwa kukamilika Machi 2027 na kunufaisha zaidi ya wananchi milioni 2.8.
Amesema sambamba na hilo Serikali inaendelea kuunganisha taasisi za umma kwenye mtandao wa Serikali, kuboresha vituo vya data (Data Centres), na kuanzisha vituo vya ubunifu ili kuharakisha mapinduzi ya kidijitali nchini.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mhe. Moshi Selemani Kakoso, ameishauri Serikali kuharakisha upanuzi wa Mkongo wa Taifa kufikia nchi jirani ya DRC ili kuongeza ushindani na manufaa ya kiuchumi.
Zaidi ya wananchi milioni 8.5 hususan wa mipakani na vijijini wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za mawasiliano kufuatia uzinduzi wa minara hiyo 758.


















