Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mara, Mhe. Ghati Zephania Chomete, ameshiriki ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo, Mifugo na Uvuvi iliyofanyika jijini Tanga, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa maendeleo ya sekta ya viwanda nchini.
Ziara hiyo imelenga kujionea hali halisi ya uzalishaji viwandani, tathmini ya mchango wa sekta ya viwanda katika uchumi wa taifa, pamoja na kubaini changamoto zinazokwamisha ufanisi wa uzalishaji.
Katika ziara hiyo, Kamati ilitembelea viwanda vitatu vikubwa vilivyopo jijini humo ambavyo ni Tanga Cement PLC, Yogi Polypack Ltd na Neel Kanth Chemical Ltd, ambapo wajumbe walijionea mchakato wa uzalishaji, ubora wa bidhaa, pamoja na mchango wa viwanda hivyo katika kutoa ajira na kukuza mnyororo wa thamani.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Ghati Chomete alieleza umuhimu wa kuendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya viwanda ili kuongeza tija, kuchochea ukuaji wa uchumi, na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
Ziara hiyo imehitimishwa kwa Kamati kutoa pongezi kwa viwanda vilivyotembelewa kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi ya Mkoa wa Tanga na taifa kwa ujumla, huku ikisisitizwa kuendelea kuboresha mazingira rafiki ya uzalishaji viwandani.





.jpg)

