Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip
Mpango amesema katika kumuenzi Jenerali Mstaafu David Musuguri inapaswa
Watanzania wote yaani askari na raia kujitoa, hata ikibidi kufa kwa ajili ya
kulinda na kutetea uhuru, heshima na maslahi ya Taifa.
Makamu wa Rais amesema hayo leo Novemba 01-2024 wakati wa kuaga mwili wa Mkuu wa Majeshi
Mstaafu, Jenerali David Bugozi Musuguri katika viwanja vya Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo
Jijini Dar es salaam.
Ametoa rai hasa kwa vijana wa Tanzania kuipenda nchi
na jeshi la Tanzania kwa moyo wote na kuwa tayari kuilinda Tanzania kwa
gharama yoyote kama alivyofanya Jenerali (Mstaafu) Musuguri.
Makamu wa Rais amesema Makamanda na Wapiganaji waliopewa dhamana
ya uongozi katika Jeshi hawana budi kuendelea kufuata mfano bora
uliyoachwa na Jenerali Mstaafu David Musuguri.
Amesema Hayati Jenerali (Mstaafu) Musuguri alilipenda sana Jeshi maisha
yake yote ambapo alitamani vijana wengi wajiunge na Jeshi na alifanikiwa sana
kuwaandikisha jeshini vijana wengi.
Amesema alikuwa mwalimu na mlezi
makini wa askari vijana.
Aidha, alipopewa jukumu la kuongoza Jeshi la
Wananchi wa Tanzania alifanya jitihada kubwa kulijenga na kuliendeleza
Jeshi na kulifanya kuwa kati ya Majeshi bora na imara barani Afrika ndiyo
maana Jeshi la Idd Amin lilipovamia kipande cha ardhi ya Tanzania lilidhibitiwa
kutoka kwa Jeshi la Tanzania likiongozwa na Jenerali Mstaafu Musuguri.
Makamu wa Rais ametoa salamu za pole Kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama
Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali nzima kwa Mkuu wa Majeshi na Jeshi la
Wananchi wa Tanzania kwa ujumla, familia, ndugu wa Marehemu na
Watanzania wote kwa msiba huu mkubwa kwa Taifa.
Amesema Serikali
inaiombea faraja familia ya hayati Musuguri na wote walioguswa na msiba
huu na kuwahakikishia kwamba Serikali na Taifa zima ipo pamoja nao.
Kwa upande wake mkuu wa majeshi wa kwanza wa jeshi la ulinzi wa wananchi Tanzania jenerali mstaafu Mrisho Sarakikya,amemuelezea marehemu Musuguri kuwa alikuwa nguzo muhimu katika jeshi hilo na kwamba midhamu na kujituma kwake kulimfanya apande vyeo hadi kuliongoza jeshi hilo.
Kwa upande wake Waziri wa Ulinzi na jeshi la Kujenga Taifa JKT Mh Dkt Stergomena Tax,ametoa Pole kwa mkuu wa majeshi,maafisa na wapiganaji ikiwemo familia kufuatia kifo cha jenerali mstaafu David Bugozi Musuguri na kusema taifa limepoteza mtu makini na aliipenda nchi yake na kuwaomba Watanzania kuendelea kumwombea.
Wakuu wa majeshi wastaafu wakiwemo Majenerali wastaafu Mirisho Sarakikya,Robert Mboma,George Waitara,Davis Mwamunyange na Venance Mabeyo ni miongoni mwa viongozi wa jeshi hilo walihudhiria tukio hilo.
Mbali na Majenerali wastaafu hao,Rais mstaafu Dr Jakaya Mrisho Kikwete,waziri mkuu mstaafu Jaji Mstaafu Joseph Warioba,katibu mkuu kiongozi Dkt.Moses Kusiluka pia wameshiriki kuaga mwili wa jenerali mstaafu Musuguri
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiliwakilishwa na katibu mkuu Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi,huku mkuu wa majeshi nchini jenerali JACOBO JOHN MKUNDA
akiongoza Maafisa Jenerali, Maafisa Wakuu, Maafisa wadogo na Askari wa JWTZ kuaga mwili wa Jenerali David Bugozi Musuguri (Mstaafu).
Mazishi ya mkuu huyo wa mejeshi mstaafu,aliyefariki Oktoba 29 mwaka huu katika hospitali ya Bugando jijini Mwanza,yanatarajia kufanyika Novemba 04-2024 katika kijiji cha Butiama,wilaya ya Butiama mkoa wa Mara.
















.jpg)








