Na Fesha Kinasa, Mara.
JAMII imeshauriwa kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira na uoto wa asili kwa kutenga maeneo ya kupanda miti ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo yamekuwa na athari kwa viumbe hai.
Hayo yamesemwa Novemba 6, 2024, na Mdau wa Mazingira Robinson Wangaso wakati akikabidhi Miche ya miti 150 katika shule ya Secondary Salama iliyopo Wilaya ya Bunda Mkoani mara.
Wangaso amesema kuwa, ili kuhakikisha mazingira na uoto wa asili unalindwa kwa manufaa endelevu ya Mwanadamu na viumbe hai. Ni jukumu la Wananchi wote kupanda miti na kuitunza vyema katika maeneo yao na kushiriki katika agenda ya serikali ya kuifanya Tanzania iwe ya kijani.
Ameihimiza pia Jamii kuzingatia matakwa ya serikali na Wadau wa Mazingira kwa kuachana na tabia zinazoathiri mazingira ikiwemo kukata miti ovyo, kuchoma mkaa na kulima maeneo ya vyanzo vya maji yaliyohifadhiwa kwani athari zake ni pamoja na kusababisha ukame.
Pia, ametoa wito kwa Wanafunzi katika shule za Msingi, Sekondari na vyuo mbalimbali waendelee kujenga utamaduni wa kupenda kupanda miti na kuitunza katika taasisi hizo. Kwani kutawafanya wawe mabalozi Waziri wa mazingira katika maisha yao.
Katika hatua nyingine, Wangaso amewaomba wanafunzi wa kidato cha nne shuleni hapo watakaohitimu masomo yao na kupata ufaulu wa Kati wa kusoma vyuo wasikae mitaani bali watafute fursa ya kujiunga na vyuo mbalimbali vya Kati kupata ujuzi kwa manufaa yao. Huku watakaofaulu akiwahimiza kuendelea na masomo yao ya kidato cha tano.
"Mtakaoshindwa kuendelea na kidato cha tano, msikae tu kijijini hapa bila kazi ya kufanya vipo vyuo mbalimbali tafuteni mjiunge msome fani mbalimbali. Mkipata ujuzi vyuoni utasaidia kujiajiri wenyewe na mtakaobahatika mtaweza kuajiriwa pia."amesema Wangaso.
Kwa upande Wake Makamu Mkuu wa Shule hiyo Cosmas Chegela amemshukuru Wangaso kwa kuunga mkono juhudi za serikali za utunzaji wa mazingira shuleni hapo, huku akiahidi usimamizi madhubuti wa miti hiyo.
"Tunakushukuru kwa kutuletea Miche hii ya miti, nikuhakikishie tutaitunza na kuisimamia kikamilifu na pia elimu ya utunzaji mazingira uliyoitoa kwa wananfunzi wetu naamini watakwenda kuifanya kazi kwa kutoa hamasa kwa Wazazi na walezi ili walau kila familia ipande miti na hata serikali imekuwa ikisisitiza Jambo hili muhimu."amesema Cosmas.


