Wajumbe wa Bodi ya Uongozi na Menejimenti ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumteua Dkt. Richard Joseph Masika kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji na kuahidi kumpa ushirikiano ili kufikia malengo ya serikali ya Agenda10/30.
Wakizungumza baada ya kuhitimisha Kikao cha Bodi cha Robo ya Tatu na Nne kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 kilichofanyika jijini Dodoma, baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Uongozi ya Tume wameahidi kumpa ushirikiano katika kukuza sekta ya kilimo cha umwagiliaji nchini.
Aidha wajumbe hao wamekiri kuridhishwa na namna Tume inavyofanya shughuli zake za ujenzi miundombinu ya umwagiliaji, ukusanyaji wa ada ya huduma za umwagiliaji, uendelezaji wa miundombinu ya umwagiliaji,utafiti na usanifu wa miradi ya umwagiliaji.
Dkt.Richard Joseph Masika ni Mhandisi Mshauri aliyeidhinishwa katika Uhandisi wa Miundombinu na aliwahi kuwa Mkuu wa Chuo cha Ufundi cha Arusha kuanzia mwaka 2009-2017.
Ana Shahada ya Uzamivu (Ph.D) katika uhandisi wa Miundombinu kutoka Chuo Kikuu cha Teknolojia na Uchumi cha Budapest cha nchini Hungary.
Akiwa mkuu wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Ufundi Arusha, alipanga na kusimamia maendeleo na utekelezaji wa sera na mipango iliyosababisha ongezeko la programu za masomo kutoka 6 hadi 19, ikijumuisha Matengenezo ya Vifaa vya Biomedical na Uhandisi wa Maji na Umwagiliaji.
Dkt.Masika ana uzoefu mkubwa na mtaala wa TVET na kuendesha taasisi ya TVET ambayo ilimfanya kushika nafasi mbalimbali kwenye Chama cha Jumuiya za Ufundi Afrika ikiwemo Naibu Mwenyekiti wa Afrika wa Shirikisho la Dunia la Polytechnics na Vyuo pamoja na Mjumbe wa Bodi wa Jumuiya ya Vyuo Vikuu na Polytechnics za Ufundi za Jumuiya ya Madola Afrika (CAPA) na Mwenyekiti wa Kamati ya Miradi ya CAPA.
Mafanikio mengine yaliyofikiwa chini ya Uongozi wa Dkt.Masika katika chuo cha Ufundi Arusha ni pamoja na kuanzisha Kampasi mpya ya Nishati Mbadala, yaani Kituo cha Mafunzo ya Nishati Mbadala, Utafiti na Uzalishaji wa Umeme wilayani Hai, mkoani Kilimanjaro, Shamba la Mafunzo ya Umwagiliaji huko Oljoro, Arusha na Kituo cha Mafunzo ya Ujuzi wa Viwanda kwa kushirikiana na Chama cha Makandarasi Raia wa Tanzania (ACCT) kilichopo ndani ya Chuo hicho
Dkt.Masika pia ana uzoefu mkubwa katika utayarishaji wa sera ambazo zimemfanya aitwe kwa mashauriano ndani na nje ya Nchi, ikiwa ni Pamoja na kuandaa Muundo wa Sera ya Jumla kwa Tathmini inayofanywa na NACTE na Taasisi za Ufundi zinazojiendesha kwa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET).
Kabla ya Dkt.Richard Joseph Masika kuteuliwa na Rais wa Jamhuri Ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan, kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi wa Tume Ya Taifa Ya Umwagiliaji. Kabla ya uteuzi huo, Dkt.Masika alikuwa kiongozi wa Baraza la Uongozi la Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam; Bodi ya Ushauri ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Ugavi, Maji na Usafi wa Mazingira ya Jiji la Arusha; Bodi ya Ushauri ya Shirika la Maendeleo ya Uhandisi na Utengenezaji Tanzania; na Hospitali ya St Elizabeth Arusha.



.jpeg)





