Na Fresha Kinasa.
MKURUGENZI wa Shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania (HGWT) Rhobi Samwelly amewataka wanafunzi wa kike wanaosoma kidato cha tano na kidato cha sita Katika Sekondari ya Wasichana ya Chief Ihunyo iliyopo Wilayani Butiama Mkoani Mara kusoma kwa bidii, kujisimamia na kujitambua ili watimize ndoto zao.
Rhobi ambaye amekuwa akijishughulisha na kutetea haki za wanawake na watoto kupitia Shirika analoliongoza, ameyasema hayo Octoba 30, 2024, wakati akizungumza na Wanafunzi hao (580) shuleni hapo. Ambapo pia, ametoa elimu ya madhara ya ukatili wa Kijinsia.
Rhobi amesema kuwa, Taifa na Jamii inahitaji Wasomi wenye ujuzi na utaalamu watakaosaidia kuendelea kuleta mageuzi chanya katika nyanja mbalimbali. Hivyo amewahimiza kutumia fursa waliyonayo kwa sasa kusoma kwa bidii na kuweka nidhamu mbele kufikia malengo yao kwa ufanisi.
Ametolea mfano Taifa la Tanzania linaongozwa na Rais mwanamke Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa kiongozi bora na mahiri kitaifa na kimataifa kutokana na kusoma kwa bidii na kujitambua hadi kufika alipo kwa sasa. Ambapo amewasisitiza pia kuwa na maono ya kuwa viongozi kwa siku za usoni na maandalizi yao yaanze wakati huu kwa kujitambua thamani yao kikamilifu.
"Niwaombe mjitambue thamani yenu wakati huu mkiwa na nafasi ya kusoma, someni kwa bidii na kusimama kwa ujasiri bila kukubali vishawishi. Ninyi ni Viongozi wa baadaye na pia ni msaada kwa Jamii na Taifa letu zingatieni masomo yenu na kuwa na malengo kila mmoja wenu."amesema Rhobi Samwelly.
Pia, Rhobi amewataka wanafunzi hao, kuwa mabalozi wazuri wa kutoa elimu ya ukatili wa Kijinsia kwa wengine. Huku akiiomba Jamii kuwawezesha Watoto wa kike kwa kuwapa mahitaji yao ya msingi na kuweka mazingira wezeshi ya wao kufikia ndoto zao.
Kwa upande wake Janeth Peter Mwanafunzi wa Kidato cha Sita shuleni hapo akizungumza kwa niaba ya wanafunzi hao, amemshukuru Rhobi Samwelly kwa kupata fursa ya kuzungumza nao na kuwatia moyo jambo ambalo amesema limewapa ari na molari ya kijituma ili watimize ndoto zao.
Naye Madame Gisela Kimario amesema kuwa, hatua ya Rhobi Samwelly kuwapa elimu ya ukatili wa Kijinsia na kujitambua itawasaidia wanafunzi hao kusimama katika malengo yao na kuwa na uchungu wa kufanya vizuri katika mitihani na masomo yao.



