Na NIRC ;Ruvuma
Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imekabidhi mtambo wa umwagiliaji wenye thamani ya shilingi millioni 4.2 kwa Jacob Davis na wenzake wawili wanaojishughulisha na kilimo cha umwagiliaji kwenye kijiji cha Nakahengwa halmashauri ya wilaya Songea Mkoani Ruvuma.
Wakulima waliokabidhiwa Mtambo wamejikita kuzalisha vitunguu ambapo Tume hiyo imetoa Mtambo huo ikiwa ni Utekelezaji wa ahadi ya Waziri wa kilimo Mhe.Hussein Bashe.
Waziri Bashe alitoa ahadi ya kuwasaidia vijana hao septemba 17 mwaka huu alipotembelea shamba lao akiwa ameongozana na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Raymond Mndolwa pamoja viongozi wengine.
Akiwa kwenye shamba hilo,Waziri Bashe alivutiwa na kilimo cha vitunguu ambapo vijana hao walieleza changamoto zinazowakabili katika kilimo hicho ikiwemo ukosefu wa miundombinu ya uhakika ya umwagiliaji,hali inayochangia kushindwa kutanua wigo wa kulima mashamba makubwa kutokana na hali duni ya kiuchumi.
Baada ya Waziri Bashe kuelezwa changamoto hiyo alimwagiza Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Raymond Mndolwa kuwanunulia vijana hao mtambo ambao umekamilika kila kitu,agizo ambalo limetekelezwa na Tume hiyo ambayo imewapatia vijana hao mtambo wenye thamani ya zaidi ya millioni nne.
Akikabidhi vifaa hivyo kwa niaba ya Waziri wa kilimo Mhe. Hussein Bashe Mkuu wa wilaya ya Songea Mhe. Kapenjama Ndile amewataka vijana hao kuvitumia kwa malengo yaliyokusudiwa hususan kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ili kuongeza tija kwenye uzalishaji wa vitunguu.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo,Mhandisi Umwagiliaji mkoa wa Ruvuma Lucy Chaula amesema mtambo huo umejumuisha Engine diesel 24 HP- pc 1, Water pump -pc 1, Delivery pipe 300m, Sunction pipe, pamoja, Sprinkler -pc 1, Cremps pamoja na Reli za engine- pc1.
Awali wakulima hao vijana walikuwa wakilazimika kutumia jenereta bovu kuvuta maji ya kumwagilia shamba hilo ambalo wakati mwingine lilikuwa na changamoto ya kushindwa kuwaka na kupelekea vitunguu kushindwa kustawi kwa kukosa maji.
Kwasasa vijana hao wanalima ekari tatu za vitunguu na soko lao kubwa ni miji ya Songea na Mbinga ambapo baada ya kupata mtambo huo wameahidi kutanua zaidi shamba lao lengo likiwa ni kuvuna zaidi na hatimaye kulisha nchi nzima.
















