📍Wanafunzi wafurahia, wampongeza mbunge
Na Mwandishi Wetu, Muheza
MBUNGE wa Muheza, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), amekagua mradi wa kisima cha maji matamu katika Shule ya Sekondari ya Kwabastola.
Shule hiyo iliopo Kata ya Makole wilayani hapa, kisima kimegharimu Shilingi milioni 12 kupitia kampuni ya Mo Maji, ikiwa ni mwendelezo wa mikakati yake ya kusogeza huduma za kijamii karibu na wapiga kura wake tangu aingie madarakani mwaka 2020.
Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo Leo Mei 29, 2026, Mhe. Mwinjuma alionyesha kufurahishwa na kukamilika kwake, hasa baada ya kubainika kuwa maji hayo ni matamu na hayana chumvi, jambo linaloyafanya yafae kwa matumizi ya shule na wananchi wa jirani.
"Wakati wa kampeni zangu, miongoni mwa ahadi kubwa nilizotoa ni kuhakikisha natatua kero ya dharura ya maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo letu. Kupatikana kwa maji haya matamu hapa Kwabastola ni ushahidi kuwa tunatekeleza Ilani kwa vitendo ili kuwasaidia watoto wetu wasome kwa utulivu," alisema MwanaFA.
*Mabweni na Vyoo vya Kisasa Kunusurika*
Naye Ofisa Mtendaji wa Kata ya Makole, Rose Maghembe, alimshukuru Mbunge huyo kwa uamuzi wake wa kuchimba kisima hicho, akieleza kuwa shule hiyo ilikuwa inakabiliwa na wakati mgumu kutokana na uwepo wa majengo mapya yasiyo na maji.
"Tunashukuru sana Mbunge wetu kwa kisima hiki. Shule yetu ina mabweni ya wasichana na wavulana ambayo yana vyoo vya kisasa vya ndani ambavyo kitalamu vilikuwa haviwezi kuishi au kutumika bila maji. Upatikanaji wa maji haya sasa unakwenda kuwasaidia wanafunzi na wananchi wa jirani na shule," alisema Mtendaji huyo.
*Maandalizi ya Kidato cha Tano Julai*
Akiwasilisha taarifa fupi ya shule kwa niaba ya Mkuu wa Shule hiyo, Juma Rashid Mdachi, Makamu Mkuu wa Shule, Lilian Godlisten Massawe, alisema miundombinu hiyo ya maji imekuja wakati muafaka kuelekea upokeaji wa wanafunzi wapya wa kidato cha tano.
Lilian alianika takwimu zinazoonyesha kuwa shule hiyo kwa sasa ina jumla ya wanafunzi 283, wakiwemo wavulana 132 na wasichana 151 waliopo kidato cha tatu, wakisoma katika mikondo miwili kwa kila kidato chini ya usimamizi wa walimu 13.
Aliongeza kuwa, mwezi ujao wa Julai (Mwezi wa Saba), shule hiyo inatarajia kupokea kwa mara ya kwanza wanafunzi wapya wa gredi ya juu wa Kidato cha Tano (High School) kwa michepuo ya tahasusi za Sayansi (CBG) na Sanaa (HGfa), hivyo kisima hicho kitasaidia kuondoa changamoto kubwa ya ukosefu wa maji.







Comments
Post a Comment