Na, Saleh Lujuo-Dodoma
KATIKA Jitihada za Kudhibiti ndege waharibifu wa Mazao ya Wakulima pamoja na visumbufu vya mazao, Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imenunua ndege nyuki za kisasa kwa ajili ya kuboresha ufuatiliaji na udhibiti wa visumbufu vya mazao mashambani ikiwa ni hatua ya kudhibiti visumbufu hivyo kabla havijasababisha madhara kwa wakulima.
Hatua hiyo inalengo kumfanya Mkulima Kuvuna mazao yake kwa Tija na kuyafanya mazao hayo kuwa Bora ili kupata soko lenye uhakika ndani na nje ya nchi.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Prof. Joseph Ndunguru ameyasema hayo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu masuala yanayohusiana na taasisi hiyo leo Machi 24, 2026, katika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) uliopo katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.
Amesema Mamlaka hiyo kwa sasa wana jumla ya ndege nyuki 21 na wako katika hatua za kukamilisha ununuzi wa ndege nyuki zingine 20.
"hatua hii itafanya idadi ya ndege nyuki kufikia 41. na ndege hizi aina ya Havilland zitatumika kupita katika mashamba ya wakulima kwa ajili ya kuchunguza viashiria vya visumbufu". Amesema
Amesema baadhi ya ndege hizo zina uwezo wa kunyunyizia viuatilifu katika eneo la hekta 52 kwa saa ambapo amesema kuwa Mamlaka hiyo imenunua ndege ya kisasa ya kunyunyizia viuatilifu aina ya Thrush 510 yenye uwezo wa kubeba lita 1,930 za viuatilifu na tenki la mafuta la lita 863.
"Ndege hiyo ina uwezo wa kunyunyizia viuatilifu katika eneo la ekari 2,400 kwa wakati mmoja na ni ya kipekee katika ukanda wa Afrika Mashariki na taratibu zote za usajili wake zimeshakamilika ikiwemo kupata ithibati kutoka serikalini". Amesema
Sambamba na hayo, Prof. Ndunguru amesema Mamlaka hiyo imeendelea kupanua wigo wa kufungua masoko mapya ya mazao ya kilimo katika nchi mbalimbali zikiwemo za bara la Afrika na mabara mengine ili kuwainua wakulima na kuongeza pato la Taifa.
"Mamlaka kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ubalozi wa Tanzania nchini China na Serikali ya Jamuhuri ya watu wa China, imefanikiwa kuratibu na kuwezesha usajili wa Makampuni 408 ya Tanzania katika mfumo wa Mamlaka Kuu ya Forodha China, General Administration of Customs of China,(GACC) na kuruhusiwa kusafirisha mazao mbalimbali ya kilimo kwenda soko la China". Amesema
"Tuna mazao mengine ambayo yapo kwenye hatua mbalimbali za kufunguliwa masoko katika nchi mbalimbali ikiwemo ndizi (Afrika Kusini) maembe (Saudi Arabia, Oman, Kuwait) maua ya Tagetes sp (Afrika Kusini, Marekani, Veitnam) na Maua ya Roses (Umoja wa Ulaya)”, ameongeza
Kadhalika,Prof. Ndunguru amesema Mamlaka hiyo imekamilisha nyaraka za kufungua masoko mapya ya mazao 14 ili kuzindua michakato ya “pest risk analysis” katika nchi 15 zitakazowezesha kufungua masoko ya mazao hayo yakiwemo ya pilipili manga, vanila, karafuu, nanasi, viazi mviringo, tumbaku, parachichi, ndizi, makadamia, ngano, maua aina ya chrysanthemum na hiliki.
Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA imedhamiria kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wadogo na wa kati wakiwemo vijana na wanawake ambapo Mamlaka hiyo imeshiriki kuwezesha kusainiwa kwa mkataba wa biashara baina ya Tanzania na Malawi kwa ajili ya nchi hizo unaohusisha bidhaa 61 ambapo kati ya hizo, 30 ni za mazao ya kilimo ikiwa ni biashara iliyolenga kuwanufaisha zaidi vijana na wanawake wa pande mbili za nchi.




