WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Isimani, Mheshimiwa William Lukuvi atakumbukwa kwa mengi na Watanzania kutokana na utumishi wake uliotukuka katika nafasi mbalimbali alizohudumu.
“Mheshimiwa Lukuvi atakumbukwa kwa mengi na Watanzania kutokana na utumishi wake uliotukuka katika nafasi mbalimbali. Mchango wake kwa Jamii na Watanzania kwa ujumla katika nafasi mbalimbali alizotumikia kuanzia Chama, Jimboni na Serikalini umekuwa chachu katika kuleta maendeleo kwa wananchi,” amesema Waziri Mkuu ambaye ameongoza mazishi hayo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumanne, Machi 31, 2026) wakati akizungumza katika ibada ya mazishi ya marehemu iliyofanyika nyumbani kwake kwenye kijiji cha Idodi, wilayani Iringa, mkoani Iringa.
"Kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan nitumie nafasi hii kuwahahikishia kwamba jinsi alivyokuwa pamoja nanyi wakati wa uhai wake, na yale yaliyokuwa ndoto yake, yataendelea kutimizwa.
"Ni vema tukizingatia na kuyaishia yale tuliyoelezwa na viongozi wa dini pamoja na kwenye wasifu wake. Alikuwa akisisitiza ushirikiano baina ya Bunge na Mawaziri, leo hii tuyaenzi yote aliyoyasimamia."
Na kwa wana-Isimani, ninawasihi tuendelee kumuenzi, tusianze mashindano, tulinde heshima ya Mzee wetu kwa kuwa na staha."
Amesema Mheshimiwa Lukuvi alikuwa anajali maisha ya wale anaowaongoza na ndiyo maana ameweza kudumu jimboni kwa miaka 31. "Sisi wanasiasa tunajua, siyo kazi rahisi kuongoza kwa muda wote huo, lakini yeye aliweza kwa sababu aliweka kipaumbele chake kwenye maisha ya wale anaowaongoza."
Amesema Serikali itaendelea kumuenzi kwa kuendelea kutekeleza miradi aliyoiacha hasa wa barabara ya lami ambayo alikuwa anaifuatilia sana. "Miradi ya Pawaga na Isimani yote itakamilishwa. Niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kuitekeleza kama sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM lakini pia sehemu ya kumuenzi Mheshimiwa Lukuvi," amesema.
Naye Spika wa Bunge la Tanzania, Mussa Azzan Zungu alisema kifo cha Mhe. Lukuvi kimeacha majonzi kwa kila mmoja na kwa uzito wa msiba huo, Bunge limewakilishwa na wabunge 160.
"Mheshimiwa Lukuvi alikuwa anaujua uwezo wake na kifo chake ni pigo ambalo Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepata kwa kuukosa umahiri wake Bungeni.
Mapema, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Stephen Wasira alitumia fursa hiyo kuwaasa vijana wa CCM wajifunze na waige mapito ya Mhe. Lukuvi ambaye alianzia ngazi za chini kabisa hadi akafika kwenye uongozi wa Taifa.
"Mwaka 1974 alijiunga na chama cha TANU, akajiendeleza hadi kufikia nafasi ya Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana."
Alisema jambo kubwa la kujifunza kutoka kwa Mhe. Lukuvi ni jinsi alivyoweza kulea jimbo ilhali ana majukumu makubwa ya kitaifa. "Siyo wengi ambao anakuwa Mbunge au Waziri halafu analea jimbo. Watu aina hii wako wachache sana. Wengi wakipata vyeo wanasahau majimbo na kuja kuwaona wapigakura wakati wa uchaguzi," alisema na kushangiliwa.
Alisema kuweza kudumu kwenye madaraka na Marais wanne tangu awamu ya Rais Mkapa hadi sasa, ni ishara tosha kwamba aliaminiwa na kuna jambo la kujifunza kutoka kwake. "Marais wote hawa walikuwa na watu wao, lakini kwa kuendelea kuwa naye, ina maana alikuwa na sifa na uwezo."
Ibada ya mazishi iliongozwa na Naibu Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa, Padre Paul Msombe ambaye alisisitiza kuwa ni vema kwatu wakaishi huku wakijiandaa kwa maisha ya baadaye mbinguni.
Akimzungumzia marehemu Lukuvi, Padre Msombe alisema: “Licha ya vyeo vyake alikuwa na unyenyekevu na mwenye kushirikiana na waumini wenzake.
Tukumbuke kwamba ipo siku tutalala usingizi kama ndugu yetu William alivyolala usingizi wa amani. Kitu cha msingi ni kujiweka mikononi mwa Mungu, tufe katika BWANA. Hili ni suala la kila mmoja kujitazama na kujihoji kwamba mimi Mungu akiniita sasa hivi, ninaweza kusema nina haki ya kuingia mbinguni.?”
Mheshimiwa Lukuvi alifariki dunia Machi 25, 2026 wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Benjamin Mkapa.










