Na Mwandishi wetu GMTV Musoma
KATIKA kipindi hiki ambacho fursa za elimu zinazidi kuongezeka nchini,Vijana wametakiwa kuzingatia kuchagua kozi wanazozipenda ili kuongeza uwezekano wa kufanikiwa kitaaluma na katika ajira huku wakisisitizwa kuwa na nidhamu ambayo itawasaidia kufikia Malengo yao.
Akizungumza katika hafla ya mahafali ya kidato Cha sita katika shule ya secondari ya Ufundi ya Musoma iliyopo Manispaa ya Musoma mkoani mara,Mhandisi mwandanizi wa Tanroads mkoa wa Mwanza Eng, Magesa Mwita,amesema kuwa wanafunzi wengi wanaokosa mafanikio hufanya hivyo kwa sababu ya kusoma kozi zisizoendana na vipaji na shauku zao.
Amesema hali hiyo husababisha kushuka kwa ari ya kazi na kufanya iwe vigumu kwa wahitimu kuendelea kukua katika taaluma zao.
“Ni bora ukasoma kozi unayoipenda hata kama ni katika chuo usichokipenda, kuliko kusoma kozi usiyoipenda katika chuo unachokipenda,” alisisitiza.
Aidha, amebainisha kuwa pamoja na uchaguzi sahihi wa kozi, bidii ni jambo lisiloweza kuepukika ambapo amesema Alama nzuri, ndiyo msingi wa kupata nafasi vyuoni na baadaye ajira, huku akiwahimiza wanafunzi kujituma tangu wakiwa shuleni.
Sambamba na hilo,Eng Magesa ameahidi kusaidia upatikanaji wa matofali kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya mwalimu, ikiwa ni sehemu ya kuboresha miundombinu ya elimu na mazingira ya kufundishia.
"Naahidi kuchangia matofali 1000 Kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za waalimu, lakini pia katika kutatua changamoto ya ukosefu wa mipira ya michezo nitatoa mipira minne katika shule hii". Amesema
Wakisoma Risala katika hafla ya mahafali hayo wanafunzi wa kidato Cha sita akiwemo Anorld wameweka wazi changamoto zinazohitaji macho na msaada zaidi ili shule izidi kupiga hatua ambapo changamoto hizo ni kujengwa Kwa uzio wa shule, uhaba wa thamani za maktaba, upungufu wa vifaa vya maabara na vyumba vya maabara, upungufu wa bwalo kutokana na wingi wa wanafunzi, huku wakiahidi kufanya vizuri katika mtihani wao wa Taifa.
Kwa upande wake Mkuu wa Shule hiyo, Mwalimu Magita Nyangore amesema mikakati waliyonayo ni kuondoa daraja la tatu na la nne na kuhakikisha idadi kubwa ya wanafunzi wanapata daraja la kwanza na la pili katika mitihani ya kidato cha kwanza hadi cha sita.
"Tunaamini kuwa wanafunzi walioandaliwa vizuri, walioelimishwa kwa umakini na maadili mema, wanaweza kufanikisha malengo haya na kuonyesha ushindi wa kweli katika elimu.”. Amesisitiza
Naye Kaimu Mwenyekiti wa shule Titus Chacha ametumia hafla hiyo kuwasisitiza wanafunzi hao kuwa na nidhamu ambapo nidhamu ndiyo uti wa mgongo wa mafanikio huku akiwasihi kufanya vizuri kwa kiwango cha juu ili waje kuwa viongozi wanaojitambua.
"nidhamu ndiyo msingi wa mafanikio na kuwa vijana hao wanapaswa kuendelea kuwa mfano bora wanapoelekea kufanya mitihani yao ya mwisho". Amesisitiza
Nao wazazi waliohudhuria katika Mahafali hayo akiwemo Enock Mgeta amewakumbusha wahitimu hao kuwa dunia ya nje haina ulinzi wa shule ni wao wenyewe na maamuzi yao ambapo amewakumbusha bidii ni jambo la msingi katika maisha yao huku Teddy Sadick akiwasisitiza wanafunzi hao kuwa waadilifu na nidhamu kwani serikali inahitaji kuwa na wafanyakazi waadilifu, wenye kufata miiko ya Kitanzania pamoja na wafanya kazi watiifu.
Mahafali ya kidato Cha sita katika shule ya Secondary ya Musoma take ni mahafali ya 55 tangu kuanzishwa Kwa shule hiyo ambapo shule hiyo imedhamiria kuondoa daraja la tatu na la nne na kuhakikisha idadi kubwa ya wanafunzi wanapata daraja la kwanza na la pili katika mitihani ya kidato cha kwanza hadi cha sita.























