Maafisa na Askari wa Hospitali ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania Kanda ya Tabora (ZMH-Tabora)iliyopo Kambi ya Mirambo wametembelea vituo vya kutunza watu wasiojiweza vya Igambiro na Charity Missionary Sisters of Tabora vilivyopo katika Halmashauri ya Manispaa Tabora, Mkoani Tabora tarehe 18 Machi 2026.
Ziara hiyo imefanyika kwa dhumuni la kuwafariji watoto wanaotunzwa kwenye kituo cha Igambiro ambao walipata Janga la Kuunguliwa Bweni katika kituo hicho na kusababisha watoto idadi 04 kupoteza maisha.
Licha ya kutembelea Watoto hao, pia walitembelea wazee, watoto na wenye uhitaji maalumu katika kituo cha Charity Missionary Sisters of Tabora.
Akizungumza kwa niaba ya Kamanda Kikosi Luteni Kanali Fredrick Maeda, Afisa Ugavi wa Kikosi cha ZMH Tabora Meja Stadius Rwiza alisema dhumuni la kutembelea vituo hivyo ni kuwaona, kutoa salamu na kuwapa mkono wa pole na kuwatia moyo kwa changamoto wanazopitia watoto hao baada ya bweni kuungua.
“Tunajua mna mahitaji mengi lakini sisi kama watoa huduma tiba tumeona tuje kuwapatia ujumbe wenye maneno ya faraja na upendo ili msione kama mmetengwa na Jamii” alisema Meja Rwiza.
Hospitali ya Jeshi ya Kanda Tabora (ZMH-TABORA) imewaletea zawadi kama Ishara ya kuwatakia Kheri ya Sikukuu ya Idd el fitri na Pasaka ili tusherehekee sikukuu kama Watu wengine waliopo maeneo mbalimbali.
Maafisa na Askari wa Hospitali hiyo wametoa msaada wa kibinadamu ikiwemo Sukari, Mchele, Mafuta ya kula, Mafuta ya kupaka pamoja na vinywaji baridi kwa kundi hilo la watoto ili wasijione wapweke katika kipindi hiki cha kuelekea Sikukuu.
Hospitali ya Kanda Tabora imekuwa na utamaduni wa kushiriki katika shughuli za kijamii pamoja na kutoa misaada ya Kibinadamu ili kuendelea kudumisha mahusiano kati ya Jeshi na taasisi mbalimbali za serikali, taasisi binafsi na wananchi ili kwa pamoja waweze kushirikiana katika kuimarisha Ulinzi Mkoani Tabora.
Licha ya kuwa na jukumu la msingi ambalo ni Ulinzi wa Mipaka ya nchi, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limekuwa na utaratibu wa kuwatembelea na kutoa misaada ya kibinadamu na huduma kwa watu wenye uhitaji na jamii kwa ujumla katika maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi wakati wa amani na operesheni mbalimbali.





