MKUU wa Wilaya ya Kyerwa, Zaitun Msofe, amewataka madiwani wa Halmashauri ya Wilaya hiyo kuongeza nguvu katika kudhibiti magendo ya kahawa na mianya yote inayosababisha Halmashauri kukosa mapato, akisema vitendo hivyo vinadhoofisha uchumi wa Wilaya na Taifa kwa ujumla.
Msofe alitoa agizo hilo jana wakati akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, kilichojadili utekelezaji wa shughuli za robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Alisema Kyerwa ipo katika msimu wa biashara ya kahawa, zao ambalo ni tegemeo kubwa kwa wakazi wa Wilaya hiyo na chanzo muhimu cha mapato ya Halmashauri, hivyo madiwani wanapaswa kufuatilia kwa karibu biashara zinazoendelea katika kata zao na kuhakikisha wafanyabiashara wanatimiza wajibu wa kulipa ushuru.
“Tuko katika kipindi cha msimu wa biashara hii ambayo tunaitegemea sana Kyerwa katika kukusanya mapato,Kahawa ndiyo zao kubwa tunalolitegemea hapa kwetu hivyo madiwani nawakumbusha kuwa wapo baadhi ya watu wanaofanya biashara hii na kukwepa kulipa ushuru wa Serikali kwa kuvusha kahawa na kuuza kwa majirani zetu,” alisema Msofe.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya alisema amepokea taarifa za baadhi ya wakulima kukusanya kahawa na badala ya kuipeleka katika Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS), wanakwenda kuiuza kwa watu binafsi wanaoweka mizani majumbani kinyume cha utaratibu.
“Ningependa tushirikiane kuhakikisha hatufanyi hujuma kwa hizi AMCOS zikakosa kahawa na matokeo yake zikafa. Pia tuangalie kwamba hatuendi kuua mnada,” alisema.
Msofe alisema baadhi ya AMCOS za maeneo ya mpakani zimeruhusiwa kununua kahawa kwa fedha taslimu kwa sababu maalumu, lakini akasisitiza kuwa utaratibu huo hautakiwi kutumiwa na wafanyabiashara wote kwa sababu unaweza kudhoofisha mfumo wa minada.
“Kabla ya mnada bei ilikuwa chini na kahawa haikuwa na thamani tukiruhusu kila mtu kununua kwa fedha taslimu, tunaua mnada na mnada ukifa, kinachofuata ni kuua bei ya kahawa kwa sababu kila mwenye pesa atanunua kwa bei anayoijisikia,” alisema.
Katika hatua nyingine, Msofe aliwataka madiwani kufuatilia kwa karibu miradi mbalimbali inayotekelezwa na jamii katika maeneo yao, akisema baadhi ya miradi imekuwa ikikabiliwa na changamoto katika utekelezaji.
Alisema fedha zinazotumika katika miradi hiyo ni fedha za umma, hivyo ni muhimu kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa kuzingatia thamani halisi ya fedha na kuleta manufaa yaliyokusudiwa kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, Bahati Henerico, alisema Halmashauri hiyo imefanikiwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Alisema Halmashauri imekusanya na kupokea Sh bilioni 51.1, sawa na asilimia 108 ya lengo la Sh bilioni 47.1, fedha ambazo zimetumika katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali, ikiwemo miradi ya maendeleo hadi Juni 2026.
Henerico alisema mapato ya ndani yamefikia Sh bilioni 7.9, sawa na asilimia 101, ikilinganishwa na lengo la Sh bilioni 7.7 ambapo mafanikio hayo yametokana na jitihada mbalimbali zilizochukuliwa na Halmashauri katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kuhakikisha vyanzo vyote vinachangia ipasavyo.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, Jemsi John, alimshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayowanufaisha wananchi huku akiwashauri madiwani kuendelea kutoa ushirikiano kwa uongozi wa Halmashauri ili kufikia malengo ya kuwapatia wananchi huduma bora na stahiki.
Kwa upande wao, baadhi ya wakulima na wananchi wa Kyerwa wameishauri Serikali kuweka mkakati wa kuhakikisha wakulima wanapowasilisha kahawa zao kwenye AMCOS wanalipwa kwa wakati, badala ya kuambiwa wasubiri malipo kwa muda mrefu wakati huo wakikabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji fedha.
Rachel Mukama, mmoja wa wananchi, alisema elimu kwa wakulima na wananchi kuhusu madhara ya utoroshaji wa kahawa ni muhimu, sambamba na kuboresha bei ya zao hilo ili kuwafanya wakulima kuona faida ya kuuza kupitia mfumo rasmi.
Alisema uzoefu wa nchi jirani unaonyesha kuwa bei nzuri inaweza kuwa kichocheo muhimu cha kuwafanya wakulima kuuza kahawa kupitia njia halali na kuongeza mapato kwa Serikali na wananchi.







Comments
Post a Comment