Wazazi na walezi wametakiwa kuwalea watoto wao kwa kuzingatia maadili mema na kuhakikisha wanadhibiti matumizi ya simu na teknolojia nyingine, ambazo zinatajwa kuwa na madhara makubwa endapo zitatumiwa bila udhibiti. Akizungumza wakati wa mahafali ya 12 ya Shule ya Msingi Waja, Mkurugenzi wa Makampuni ya Waja, Chacha Wambura, alisema kuwa ni jukumu la wazazi na walezi kuhakikisha watoto wanapata malezi bora yanayowajenga kuwa raia wema. Ameongeza kuwa matumizi mabaya ya simu na teknolojia, hasa mitandao ya kijamii, yanaweza kuwa chanzo cha tabia zisizofaa miongoni mwa watoto. “Mazingira ya sasa yanahitaji wazazi kuwa makini zaidi. Tunapaswa kuwaelekeza watoto wetu matumizi sahihi ya teknolojia ili kuepuka madhara yanayoweza kusababisha athari mbaya kwa ukuaji wao,” alisema Chacha Wambura. Mgeni rasmi katika mahafali hayo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Gombati, ameeleza kuwa shule za Waja zimeendelea kuwa mfano mzuri katika kutoa elimu bora na kuwalea watoto katika mising...