WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na mwenyeji wake Waziri Mkuu wa Grenada, Dickon Thomas Mitchell na kumhakikishia kuwa Tanzania itaendeleza mahusiano kidiplomasia na kibiashara kwa manufaa ya pande zote mbili.
Amesema kuwa Tanzania itaendelea kutumia Jukwaa la Nne la Kibiashara na Uwekezaji kati ya Afrika na Karibiani (ACTIF2025) kama daraja la kukuza ushirikiano katika maeneo ya kipaumbele yakiwemo kilimo, uvuvi, afya na elimu ili kuwanufaisha wananchi wa pande zote mbili.
Katika mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa mwenyeji wake jijini St. George’s, Grenada, Waziri Mkuu Majaliwa alisisitiza kuwa Tanzania iko tayari kushirikiana na Grenada na kubadilishana uzoefu katika teknolojia na maarifa ya kitaalamu hususan katika sekta za uzalishaji na huduma ili kuimarisha uchumi wa viwanda na kuongeza ajira kwa vijana.
Kwa upande wake, Mheshimiwa Mitchell alisema kuwa malengo ya nchi hiyo kupitia jukwaa la ACTIF ni kuhakikisha kuwa nchi za Karibiani na Afrika, zikiwemo Tanzania na Grenada, zinajenga misingi imara ya kiuchumi kwa kukuza biashara ya pande mbili katika maeneo mbalimbali.
Viongozi hao walikubaliana kuendelea kuhimiza majadiliano ya kiserikali baina ya nchi hizo mbili na kushirikiana kwa karibu kufanikisha mikakati ya pamoja ya maendeleo, huku wakisisitiza umuhimu wa mshikamano baina ya watu wa Afrika na Karibiani kama msingi wa ustawi wa kiuchumi na kijamii.
Mheshimiwa Waziri Mkuu ameambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji wa SMZ, Bw. Shariff Ali Sharriff na Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Cuba, Karibe, Marekani ya Kati na nchi za Venezuela na Guyana, Bw. Wilbroad Kayombo.