Na,Saleh Lujuo-Dodoma:
SERIKALI kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imejipanga kuongeza uwekezaji mkubwa katika ujenzi na upanuzi wa barabara nchini ili kuendana na kasi ya ukuaji wa miji, ongezeko la magari na mahitaji makubwa ya usafirishaji wa mizigo ndani na nje ya nchi.
Hatua hiyo inalenga kuboresha mtiririko wa usafiri, kupunguza msongamano wa magari na kufungua zaidi fursa za biashara katika ngazi ya ndani na kikanda.
Akizungumza leo jijini Dodoma, Kaimu Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Ephatar Mlavi, amesema serikali imeongeza rasilimali katika sekta ya miundombinu ili kuhakikisha barabara za kitaifa zinajengwa, zinaboreshwa na zinatunzwa kwa viwango vinavyoendana na ukuaji wa uchumi.
Amesema ongezeko la idadi ya magari pamoja na kuimarika kwa usafirishaji wa mizigo kutoka nchi jirani ikiwemo DRC, Rwanda, Burundi, Uganda, Malawi na Zambia, limeongeza mahitaji ya miundombinu ya barabara, hali inayolazimu serikali kuchukua hatua madhubuti za kuongeza uwezo wa barabara zilizopo na kujenga mpya.
“Serikali inaendelea kuwekeza kwa nguvu katika sekta ya barabara ili kuhakikisha inakidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye ya uchumi unaokua kwa kasi,” amesema Mlavi.
Katika kuimarisha ulinzi wa barabara, Mlavi amesema serikali imeongeza udhibiti wa uzito wa magari ili kuzuia uharibifu wa miundombinu, ambapo tayari mizani 20 ya kisasa ya kupima magari yakiwa kwenye mwendo (weigh in motion) imewekwa katika maeneo mbalimbali nchini ili kupunguza foleni na kuongeza ufanisi.
Aidha, amesema matumizi ya teknolojia yameongezwa kwa kufungwa kwa kamera za ufuatiliaji (CCTV) katika vituo 13 vya mizani, hatua inayolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na kudhibiti vitendo visivyofaa.
Akizungumzia hali ya barabara za kitaifa, Mlavi amesema takwimu zinaonesha kuwa katika kipindi cha miaka mitano hadi mwaka 2025, asilimia 30 ya barabara ziko katika hali nzuri, asilimia 57 ziko katika hali ya wastani huku asilimia 13 zikiwa katika hali mbaya.
“Kwa ujumla, asilimia 87 ya mtandao wa barabara za kitaifa uko katika hali nzuri na ya wastani, jambo linaloonesha dhamira ya serikali katika kulinda na kuendeleza uwekezaji wa miundombinu,” amesema.
Amesisitiza kuwa barabara ni mhimili muhimu wa uchumi wa taifa, akibainisha kuwa kati ya asilimia 80 hadi 90 ya usafirishaji wa mizigo na abiria nchini unategemea barabara, hivyo uwekezaji unaoendelea utakuwa chachu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi.




